Serikali yapendekeza kuondoa ada vyuo vya ufundi Tanzania
- Ni kwa ajili ya kuongeza wataalamu wenye ujuzi kuchochea mapinduzi ya viwanda.
- Vyuo vinavyopendekezwa ni DIT, MUST, pamoja na ATC.
Dar es Salaam. Serikali inakusudia kuondoa ada katika ngazi ya elimu ya kati kwa baadhi ya vyuo vya umma nchini ili kuongeza idadi ya wataalamu wenye ujuzi unaohitajika katika mapinduzi ya viwanda yanayotarajiwa kuwa gurudumu la uchumi.
Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Mwigulu Nchemba amewaambia wabunge jijini Dodoma kuwa katika jitihada za kuondoa ada kwa wanafunzi nchini anapendekeza sasa kuwaondolea karo wanafunzi watakaochaguliwa na Serikali kujiunga vyuo vya ufundi.
Katika hotuba yake ya bajeti, Dk Nchemba vyuo vinavyopendekezwa kufutiwa ada ni Dar es Salaam Institute of Technology (DIT), Mbeya University of Science and Technology (MUST) pamoja na Arusha Technical College (ATC).
“Napendekeza kuondoa ada kwa wanafunzi wanaomaliza kidato cha nne na kupangiwa na Serikali kujiunga na vyuo vya ufundi vya DIT, MUST na ATC, hatua hii inalenga kuongeza idadi ya wataalamu wenye ujuzi na elimu inayohitajika katika azma hizi za mapinduzi ya nne ya viwanda,” amesema Dk Nchemba.
Soma zaidi
-
Pato la mtu Tanzania laongezeka kwa zaidi ya Sh135,000 mwaka 2022
- Deni la Serikali Tanzania laongezeka hadi Sh79.1 trilioni
- Wizara zitakazotumia bajeti kubwa mwaka 2023 – 24 Tanzania
Kwa muda mrefu wadau wa mbalimbali wamekuwa wakiishauri Serikali kuondoa ada au kuweka utaratibu wa mikopo kwa wanafunzi wanaosoma vyuo vya kati jambo ambalo Mwigulu amesema Serikali inakusudia kutekeleza mwaka 2023/24.