Serikali yaanza kuwanoa walimu kwa mafunzo ya amali
- Ni maandalizi ya utekelezaji wa mabadiliko ya Sera na mitaala ya elimu
- walimu 506 wanaofundisha wenye mahitaji maalumu kupata darasa kwa siku nne
Mwanza. Serikali imeanza kutekeleza mabadiliko ya Sera ya Elimu nchini kwa kutoa mafunzo ya amali kwa walimu ili kuwaandaa wanafunzi kuwa na uwezo wa kuajiriwa na kujiajiri pindi wamalizapo masomo yao.
Amali ni mafunzo yanayohusisha ujuzi wa ufundi na ufundi stadi katika nyanja mbalimbali ikiwemo ufundi cherehani, makenika, uashi pamoja na ususi.
Pamoja na kumuwezesha mwanafunzi kufahamu stadi mbalimbali za maisha mafunzo hayo yanalenga kuwanoa wanafunzi katika lugha ili waweze kuzungumza na kuandika kwa ufasaha Kiingereza na Kiswahili.
Mkurugenzi wa idara ya Elimu nchini Huruma Elias, aliyekuwa akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo kwa walimu 506 wanaofundisha wanafunzi wenye uhitaji maalumu amewaambia lengo la mafunzo hayo ni kuwapa ujuzi utakaowasaidia wahitimu kufanya shughuli za uzalishaji.
“Tuna mabadiliko ya sera na mitaala ambapo walimu watapatiwa mafunzo ambayo yata msaidia mtu aweze kujiajiri ambapo pamoja na mwalimu kuandaliwa kufundisha ualimu lakini awe na somo mojawapo la amali ambalo atalifundisha kwa wanafunzi,” amesema Elias
Mafunzo hayo ya siku nne yaliyohusisha walimu kutoka mikoa ya Mwanza, Kagera, Kigoma, Mara na Shinyanga ni mwendelezo wa mafunzo yaliyofanyika mwaka 2022.
Jumla ya halmashauri 144 zimeshapatiwa mafunzo hayo ambapo walimu 39,000 wa Sekondari wameshapatiwa mafunzo hayo na wa shuke za msingi ni walimu 3,799.
Selemani Idrisa ambaye ni mwalimu wa Shule ya Msingi Mkeza iliyopo Manispaa ya Bukoba amesema mafunzo hayo yamekuja kwa wakati mwafaka hasa kwa walimu walioko kazini kwani yatamfanya mwalimu aendane na kasi ya mabadiliko ya sayansi na teknolojia yaliyopo hivi sasa.
“Ni mafunzo ambayo yanaendana na wakati uliopo wa ukuaji wa teknolojia yatamfanya mwanafunzi awe wa kisasa zaidi ,”amesema Idrisa
Latest