Rais wa Tanzania azindua Ikulu mpya miaka 50 baada ya uamuzi wa kuhamia Dodoma
- Rais Samia asema safari ya kuhamia Dodoma haikuwa rahisi
- Matatizo ya kiuchumi ni miongoni mwa sababu zilizofanya mchakato huo kuchukua nusu karne.
- Ikulu ya Chamwino ni kubwa mara 200 ya ile ya Magogoni iliyopo jijini Dar es Salaam.
Dar es Salaam. Mara tu baada ya uamuzi wa Serikali kuifanya Dodoma kuwa makao makuu ya Tanzania mwaka 1973 mpango ulikuwa ni kukamilisha safari hiyo ikiwemo kujenga Ikulu ndani ya miaka 10.
Hata hivyo, safari hiyo haikuwa kutimia ndani ya muda uliopangwa hadi leo Mei 20, 2023 baada ya Rais Samia Suluhu Hassan kuzindua Ikulu mpya na ya kisasa ya Chamwino ikiwa ni miaka 50 tangu uamuzi wa kuhamia Dodoma kufanyika.
Mchakato huo wa ujenzi wa ikulu mpya ya Tanzania ulianza wakati wa uongozi wa Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere na kuendelezwa na Marais wa awamu zote zilizopita na kukamilishwa na Rais Samia.
Rais Samia amewaleza wageni waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Ikulu hiyo kuwa mchakato wa kuhamia Dodoma umechukua miaka mingi kutokana na sababu mbalimbali ikiwemo za kiuchumi.
“Kazi haikuwa ndogo ilikuwa ni kazi ya kila awamu iliyoingia madarakani kuwezesha au kuanza ujenzi wa vitu mbalimbali ili Dodoma ichukue sura ya kuwa makao makuu ya Serikali,” amesema Rais Samia.
Safari ya kukamilika kwa Ikulu hiyo ambayo ni ofisi na makazi rasmi ya Rais wa Tanzania na ujenzi wa ofisi nyingine za Serikali mkoani Dodoma ilipitia michakato mbalimbali ya kidemokrasia ya kukusanya maoni kutoka matawi mbalimbali ya Chama cha Tanu yaliyokuwepo wakati huo.
Baadhi ya viongozi waliopo madarakani na wastaafu waliohudhuria hafla ya uzinduzi wa Ikulu ya Chamwino,Dodoma.Picha|Ikulu/Twitter
Hoja ya kuhamia Dodoma iliwahi kupigwa chini
Hatua hiyo ilikuja miaka sita hivi baada ya hoja ya mdogo wa Baba wa Taifa na aliyekuwa Mbunge wa Musoma, Joseph Nyerere ya kutaka makao makuu yawe Dodoma, kupigwa chini bungeni mwaka 1966.
Safari hii ililetwa na kamati ya Tanu mkoa wa Mwanza na kuwasilishwa katika kamati kuu ya Tanu kwa mujibu wa Rais Samia.
Katika kura za maoni zilizokusanywa katika matawi ya Tanu wakati ule, matawi 1,017 yalikubali Dodoma kuwa makao makuu kati ya 1,859 yaliyokuwepo, hatua iliyobariki uamuzi wa kuhamishia makao makuu ya Serikali katika mkoa huo kutoka jijini Dar es Salaam.
Mwaka 1973 mara baada ya halmashauri kuu ya Tanu kuridhia, Hayati Mwalimu Julius Nyerere alitangaza rasmi kuwa mchakato huo ufanyike na kukamilika ndani ya miaka 10.
Soma Zaidi
Magufuli alichochea kasi ya kuhamia Dodoma
Hata baada ya Nyerere kuondoka madarakani viongozi waliofuata walishika hatamu kuhakikisha utekelezaji wa agizo hilo la aliyekuwa Rais wa kwanza wa Tanzania.
Wakati huo jitihada mbalimbali ziliendelea kufanyika kuboresha mji huo wa Serikali lakini ni Hayati Rais John Magufuli aliyechochea kasi ya kuhamia Dodoma. Mwaka 2016 Magufuli alitangaza rasmi Serikali kuhamia katika mji huo uliopo katikati ya nchi.
Katika kipindi cha miaka sita sasa ofisi nyingi za Serikali zimehamia Dodoma huku ujenzi wa ofisi za wizara mbalimbali zikiwa katika hatua za mwisho katika Mji wa Serikali Mtumba. 
Baadhi ya Mawaziri wa Wizara mbalimbali nchini waliohudhuria halfa ya uzinduzi wa Ikulu Chamwino, Dodoma.Picha|Ikulu/Twitter.
Ujenzi wa Ikulu wachukua miezi 30
Katika halfa iliyohudhuriwa na wageni mbalimbali wakiwemo marais wastaafu wa Tanzania na Zanzibar, Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Majengo Tanzania (TBA) Daudi Kandoro ameeleza kuwa ujenzi wa Ikulu hiyo yenye ekari 8,473 umechukua takribani miezi 30 tangu kuanza ujenzi mwaka 2020.
Eneo hilo la Ikulu ya Dodoma ni kubwa zaidi ya mara 200 ya eneo la Ikulu ya Dar es Salaam maarufu kama Magogoni lenye ekari 41.
Katika hafla hiyo, Rais mstaafu Jakaya Mrisho Kikwete amesema tukio hilo muhimu linahitimisha dhamira ya Baba wa Taifa ya kuhamishia makao makuu kutoka Dar es Salaam kuyaleta Dodoma.
“Kilele cha uamuzi ule ni Rais kuhamia Dodoma na siyo kwa kupita lakini Rais kuwa na makazi yake Dodoma,” amesema Kikwete.
Mstaafu huyo amesimulia jinsi alivyofanya uamuzi wa kuifanya Dodoma kuwa makazi na ofisi rasmi ya Rais wa Tanzania.
“Wazo lilikuja mwanzoni pale Chimwaga ndipo patakuwa makao makuu ya Chama cha Tanu na makao makuu ya Serikali…nikawaambia jambo la kufanya nendeni kuala Lumpur -Malaysia mkajifunze,” amesema.