Nukta AI, Pawa AI zaungana kuimarisha teknolojia ya lugha za Kiafrika
- Ushirikiano huu unalenga kuja na mifumo yenye uelewa wa lugha na mazingira ya Kiafrika.
Dar es Salaam. Kampuni ya habari na teknolojia ya Nukta Africa imeingia ubia na kampuni ya Sartify kuendeleza mifumo ya Akili Unde (AI) inayoweza kuelewa na kutumia lugha za Kiafrika katika bidhaa na huduma za kidijitali.
Ushirikiano huo unalenga kushughulikia changamoto ya uwakilishi mdogo wa lugha za Kiafrika katika mifumo yao ya kisasa ya AI, (Pawa AI, Nukta AI) kwa kuanza na Kisukuma kinachozungumzwa katika baadhi ya mikoa ya Kanda ya Ziwa na baadae kuzifikia lugha nyingine za asili zinazotumika Tanzania.
Daniel Mwingira, Afisa Maendeleo ya Biashara wa Nukta Africa, amesema ushirikiano huo utaiwezesha Nukta kutumia utaalamu huo katika kuendeleza bidhaa zake.
“Tunataka kutumia lugha na ubunifu zaidi kwenye bidhaa zetu, hasa za habari. Tunaweza kufikiria siku moja mtu akaingia kwenye tovuti zetu na kusoma habari katika lugha yake ya asili, kama Kisukuma, Kinyakyusa au Kihehe,” amesema Mwingira.
Mwingira ameongeza kuwa upatikanaji wa taarifa katika lugha ambayo mtumiaji anaielewa vizuri unaweza kusaidia kuongeza upatikanaji wa elimu na maarifa, hasa miongoni mwa jamii zinazotumia lugha za asili katika mawasiliano ya kila siku.
Kisukuma kupewa kipaumbele
Kwa upande wa Innocent Charles Mwanzilishi mwenza wa Pawa AI na Afisa Mkuu wa Akili Unde (AI) wa Sartify amesema moja ya changamoto kubwa katika mifumo mingi ya AI iliyotengenezwa nje ya Afrika ni ukosefu wa uelewa wa kutosha wa taarifa na muktadha wa lugha na utamaduni wa Kiafrika.
“Lugha zetu na muktadha wetu vinakosekana katika baadhi ya suluhisho zinazotoka nje. Ushirikiano huu unalenga kuja na mifumo yenye uelewa wa lugha na mazingira yetu,” ameeleza Charles.
Amesema Kisukuma ndicho kinachopewa kipaumbele katika hatua ya sasa ya ushirikiano huo, huku kampuni hizo zikitarajia kuongeza lugha nyingine kadiri taarifa zitakavyopatikana na rasilimali zinazohitajika kwa ajili ya mafunzo ya mifumo hiyo.
Kutoka maandishi hadi sauti
Mbali na maandishi, washirika hao wanaangalia pia uwezekano wa kutumia teknolojia ya sauti katika lugha za Kiafrika.
Hii inaweza kuwezesha mifumo ya AI kutambua na kuchakata matamshi ya lugha za asili, hatua ambayo itaongeza matumizi ya teknolojia hiyo miongoni mwa watu ambao hawapendelei au hawawezi kutumia maandishi kama njia kuu ya mawasiliano.
Naye Msanifu wa mifumo ya programu Abdul Karim amesema kazi ya kufundisha mifumo hiyo inahitaji ukusanyaji wa data ya lugha husika, ikiwemo maneno, tafsiri na mifano ya matumizi ya lugha katika mazingira halisi.
Amefafanua kuwa baadhi ya lugha hizo hazijawakilishwa vya kutosha katika mifumo iliyopo ya AI, hivyo kuna haja ya kufanya kazi ya ukusanyaji na uchakataji wa data kabla ya mifumo hiyo kufikia kiwango kinachohitajika.
“Lazima zoezi la kuifundisha mashine lifanyike. Hii ni kazi ambayo imefanyika kwa kiwango kikubwa na Pawa AI, hivyo tunaweza kutumia mifumo yao huku tukijifunza na kuendelea kuiboresha pamoja,” amesema Karim.
Karim amesema moja ya njia zinazoweza kutumika ni kuwashirikisha wazungumzaji wa lugha husika katika kutafsiri na kuthibitisha taarifa, pamoja na kutumia vitabu na vyanzo vingine vinavyoweza kutoa data ya lugha.
Kwa Nukta Africa na Pawa AI, lengo la ushirikiano huo ni kuhakikisha kuwa maendeleo ya akili unde yanawafikia watumiaji wa Afrika kwa lugha na mazingira wanayoyaelewa, huku yakifungua nafasi zaidi kwa lugha za Kiafrika katika uchumi wa kidijitali.