Mwanza kuongeza kasi utoaji chanjo ya Uviko-19

September 23, 2021 11:53 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Yachanja asilimia 17.7 ya dozi za chanjo ilizopokea.
  • Yaongeza vituo vya chanjo ili kuwafikia watu wengi.
  • Viongozi wa dini, Serikali kuongeza hamasa kwa wananchi.

Mwanza. Ikiwa zimepita wiki saba tangu zoezi la utoaji chanjo ya Corona (Uviko-19) lizinduliwe jijini Mwanza, ni asilimia 17.7 ya dozi za chanjo hiyo ndiyo watu wamechanjwa, huku mkoa ukijipanga kuongeza kasi ya kuchanja.

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Dk Thaomas Rutachunzibwa amesema mkoa huo ulipokea dozi 90,000 ambapo mpaka sasa umefanikiwa kutoa dozi 16,000 tu. 

Mkoa wa Mwanza ulizindua zoezi la utoaji chanjo Agosti 3 mwaka huu na jumla ya vituo 27 viliteuliwa katika halmashauri nane za mkoa huo kutoa chanjo hiyo.

Kutokana na mkoa huo kushindwa kutoa nusu ya dozi ilizopokea, imeweka mpango wa kufikia watu wengi zaidi ikiwemo kampeni za kata kwa kata. 

Dk Rutachunzibwa amesema mpango huo utasaidia kuongeza idadi ya watu watakaojitokeza kupata chanjo kuliko ilivyo sasa kwa sababu umeshirikisha viongozi wa dini , wakuu wa wilaya, wakurugenzi na wataalam wa afya.

Amesema wakati chanjo inaanza kutolewa mkoani Mwanza ilikuwa na vituo 27 na kwamba vituo vimeongezeka ambapo kwa sasa chanjo itakuwa inatolewa kwenye vituo 346 kwa wilaya zote saba za Mwanza.

“Tumepanua wigo ya utoaji chanjo kwenye maeneo, tumeongeza vituo 319 kutoka 27 ili kuwapunguzia watu kutembea umbali mrefu kufuata chanjo, tayari  watoa huduma za afya 600 wamepatiwa mafunzo kwa ajili ya kwenda kufanya kazi kwenye vituo hivyo,” amesema Dk Rutachunzibwa.

Kwa mujibu wa Dk Rutachunzibwa amesema chanjo zimegawiwa kwenye halmashauri zote ambazo pia zimeanza usambazaji kwenye  vituo na vilivyobaki ndani ya siku tatu vitakuwa vimepatiwa chanjo.

Kupitia mpango wameunda tume ambayo itakuwa na watalaam watakaokuwa wanatoa ufafanuzi kuhusu hoja zitakazokuwa zinatolewa na wananchi.

“Kupitia mpango huo hadi kufikia mwezi Desemba chanjo tulizokuwa tumepatiwa zitakuwa zimeisha na kuomba chanjo zingine,” amesema 

Hivi karibuni Serikali ya Tanzania ilitoa maagizo kwa  waganga wakuu wa mikoa na wilaya kusimamia mpango wa jamii shirikishi na harakishi wa chanjo dhidi ya Uviko-19 ili kuhakikisha kuwa chanjo za ugonjwa huo ziishe mapema.

Dozi za chanjo zilizoingizwa nchini kutoka nchini Marekani ni milioni 1.058 ambapo hadi kufikia Septemba 15 zaidi ya nusu ya chanjo hizo bado zilikuwa hazijatumika.

Hata hivyo, Serikali  imeendelea kusisitiza kuchanja ni hiari.

Askofu wa Kanisani la Kiinjili la Kirutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Ngara, Benson Bagonza amewataka wananchi kutosikiliza maneno ya upotoshaji kuhusu chanjo ya Uviko-19 kwa kuwa chanjo inayotolewa ni salama.

Amesema watu wajitokeze kwa wingi kuchanjwa ili kujikinga na kuwakinga wengine ili Taifa liwe salama dhidi ya ugonjwa huo.

Makala hii imefadhiliwa na Shirika la maendeleo ya habari la International Media Support (IMS) na Umoja wa Ulaya (EU).

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW