Mgonjwa mwingine apona corona Tanzania, wagonjwa wafikia 20
- Wizara ya afya imethibitisha mgonjwa mwingine leo.
- Mgonjwa huyo ni mwanamke raia wa Marekani mwenye miaka 42
- Mpaka sasa Tanzania imethibitisha wagonjwa 20, wawili wamepona na mmoja amefariki dunia.
Dar es Salaam. Idadi ya wagonjwa wa virusi vya corona nchini imezidi kuongezeka baada ya Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kuthibitishaa mgonjwa mpya wa maambukizi ya virusi vya Corona na hivyo kufanya idadi ya wagonjwa nchini kufikia 20.
Hata hivyo, kuna habari njema baada ya mgonjwa mwingine aliyekuwa akipatiwa matibabu jijini Dar es Salaam kupona ugonjwa huo unaosambaa kwa kasi ulimwenguni.
Taarifa ya Waziri wa wizara hiyo, Umm Mwalimu iliyotolewa leo (Aprili 1, 2020) inaeleza kuwa mgonjwa mpya ni mwanamke raia wa Marekani mwenye miaka 42.
Ummy amesema mgonjwa huyo amekuwa karibu na mtu aliyesafiri nje ya nchi na baadaye kuthibitika kuwa na maambukizi ya virusi vya COVID-19 aliporejea hapa nchini
“Hivyo hadi sasa kesi za maambukizi ya virusi vya Corona (COVID-19) zilizothibitishwa hapa nchini ni 20 ambapo wagonjwa 17 wanaendelea na matibabu na hali zao ni nzuri,” amesema Ummy katika taarifa hiyo.
Aidha, Waziri ameeleza kuwa mgonjwa mwingine wa Corona aliyekuwa akipata matibabu katika kituo cha matibabu cha Temeke jijini Dar es Salaam amethibitika kupona jana.
Amesema mgonjwa huo ameruhusiwa nyumbani na hivyo kufanya wagonjwa walioopona kuwa wawili.
Mgonjwa huyo anakuwa mgonjwa wa tatu kupona katika ukanda wa Afrika Mashariki ambao mpaka sasa umeshuhudia vifo vya wagonjwa wawili katika nchi za Kenya na Tanzania.
Zinazohusiana
Mpaka sasa mkoa wa Dar es Salaam ndiyo unaongoza kuwa na wagonjwa wengi wa Corona wanaofikia 12 ukifuatiwa na visiwa vya Zanzibar (5), Arusha (2) na mmoja alithibitishwa katika mkoa wa Kagera.
Aidha,wananchi wametakiwa kuendelea kuchukua tahadhari kujikinga na ugonjwa huu kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima, kunawa mikono mara kwa mara, kuepuka kugusa pua, macho na mdomo na kutumia tishu wakati wa kukohoa.
Takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) za hadi jana Machi 31 zinaeleza kuwa watu 750,890 wameambukizwa ugonjwa huo na kuua watu 36,405 duniani kote.