Magufuli azungumzia chanjo, maambukizi ya Corona Tanzania
- Asema hatarajii kutangaza Watanzania kujifungia ndani ili kujilinda na Corona.
- Awataka waendelea kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huo.
- Pia awatahadharisha matumizi ya chanjo ya ugonjwa huo.
Dar es Salaam. Rais John Magufuli amesema hatatangazwa Watanzania wajifungie ndani kwa sababu ya ugonjwa Corona huku akiwataka kuchukua tahadhari dhidi ya ugonjwa huo na kuendelea kumuomba mungu.
Kauli ya Rais imekujwa wakati kukiwa na mijadala mbalimbali katika mitandao ya kijamii ya kuwepo kwa maambukizi ya ugonjwa huo nchini huku baadhi ya taasisi zikiwemo za dini zikiwataka watu wake kuchukua tahadhari ya kujikinga na ugonjwa huo.
Dk Magufuli aliyekua akizungumza leo Januari 27, 2020 wakati akizindua shamba la miti wilayani Chato mkoani Geita, amesema wakati nchi mbalimbali zikikataza watu wake kutoka nje kujikinga na Corona, Tanzania haitafanya hivyo na watu wake wataendelea kuchapa kazi.
“Nchi nyingi wananchi wake watakua wamejifungia ndani, sisi Watanzania hatujajifungia ndani na hatutegemei kujifungia ndani na wala sitegemei kutangaza hata siku moja kwamba tunajifungia ndani kwa sababu Mungu wetu yuko hai na ataendelea kutulinda Watanzania,” amesema Rais Magufuli
Licha ya kutojifungia ndani, amewataka Watanzania kuendelea kuchukua tahadhari zote zinazopendekezwa na wataalam wa afya dhidi ya ugonjwa huo.
Pia amewataka kuendelea kufanya kazi kwa bidii, kuongeza kasi ya kuzalisha chakula na kufanya mazoezi yatakayowapatia nguvu za kujikinga na virusi vya COVID-19.
“Lakini pia tutaendelea kuchukua tahadhari zingine za kiafya ikiwa ni pamoja na kujifukizia huku unamuomba Mungu huku unapiga zoezi la kufanya kazi, kulima mahindi, viazi ili ule vizuri Corona ishindwe kuingia kwenye mwili wako,” amesisitiza Rais akiwa Chato.
Amesema Watanzania wameweza kukaa bila Corona kwa zaidi ya mwaka mmoja na hivyo wanatakiwa kuendelea kumuomba Mungu awapiganie na kuwalinda dhidi ya janga hilo.
Zinazohusiana:
- Jinsi ya kujikinga na virusi vya Corona kwenye mikusanyiko ya watu
- Magufuli aagiza safari za nje zipunguzwe kujikinga na virusi vya Corona
- WHO: Njia ya kumaliza Corona ni kuvunja mnyororo wa maambukizi
Azungumzia chanjo
Amewataka Watanzania kusimama imara kipindi hiki dhidi ya vitisho vyote vya ugonjwa huo na kuwa makini na chanjo za magonjwa zinazotolewa duniani ikiwemo ya COVID-19.
“Mtatishwa sana ndugu zangu Watanzania lakini simameni imara. Ninajua wako baadhi ya watanzania wameondoka ndani ya nchi na kukimbilia maeneo mengine na kwenda kuchanjwa na wametuletea Corona ambayo ni ya ajabu. Simameni imara”
“Niombe Wizara ya Afya isiwe inakimbilia mambo ya chanjo bila yenyewe kujiridhisha. Siyo kila chanjo ni amana kwa Taifa letu, siyo kila chanjo ina faida kwetu,” amesema kiongozi huyo wa nchi.
Latest