Mfumuko wa bei za bidhaa, huduma muhimu washuka Februari
- Umeshuka hadi asilimia 4.8 kutoka asilimia 4.9 ya mwaka ulioishia Januari 2023.
Dar es Salaam. Kasi ya mfumuko wa bei za bidhaa na huduma nchini Tanzania umeshuka hadi kufikia asilimia 4.8 kwa mwaka ulioishia Februari 2023 kutoka asilimia 4.9 iliyorekodiwa Januari mwaka huu.
Mfumuko wa bei wa Taifa hupima kiwango cha kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma zote zinazotumiwa na kaya binafsi nchini.
“Hii inamaanisha kuwa, kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishia mwezi Februari, 2023 imepungua ikilinganishwa na kasi iliyokuwepo kwa mwaka ulioishia mwezi Januari, 2023,” imeeleza taarifa ya NBS iliyotolewa leo Machi 9, 2023.
Mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwaka ulioishia Februari, 2023 umepungua hadi asilimia 9.6 kutoka asilimia 9.9 kwa mwaka ulioishia Januari, 2023.
“Kwa upande mwingine, mfumuko wa bei ambao haujumuishi bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwezi Februari, 2023 umepungua pia hadi asilimia 2.8 kutoka asilimia 3.0 ilivyokuwa mwezi Januari, 2023,” imeeleza NBS.
Kwa mujibu wa ofisi hiyo, mfumuko wa bei umekuwa na mwenendo imara ambao uko kati ya asilimia 3.6 na asilimia 4.9.
NBS imeeleza kuwa fahirisi za bei za Taifa kati ya Januari 2023 na Februari 2023 zimeongezeka kwa asilimia 0.4.
Kuongezeka kwa fahirisi za bei kumechangiwa na kuongezeka kwa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula na bidhaa zisizo za vyakula.
Baadhi ya bidhaa za vyakula zilizochangia kuongezeka kwa hahirisi za bei ni pamoja na ngano kwa asilimia 1.2, mtama (asimimia 0.7), ulezi (asilimia 3.3), unga wa ngano (asilimia 1.2), unga wa mtama (asilimia 1.9) na unga wa mahindi kwa asilimia 2.4.
Samaki wabichi kwa asilimia 0.4, dagaa wakavu (asilimia 0.7), matunda (asilimia 0.6), karanga mbichi (asilimia 4.4), mbogamboga (asilimia 1.7), viazi vitamu (asilimia 6.7), mihogo mibichi (asilimia 4.0) na maghimbi kwa asilimia 1.4.
Bidhaa zingine za vyakula ambazo bei zake zimepanda ni maharagwe kwa asilimia asilimia 2.8, choroko kavu (asilimia 0.8), njegere kavu (asilimia 1.0), kunde kavu (asilimia 1.0), unga wa muhogo (asilimia 5.6) na vinywaji visivyo na kilevi kwa asilimia 0.7.
Kwa upande mwingine baadhi ya bidhaa zisizo za vyakula zilizochangia kuongezeka kwa fahirisi za bei ni pamoja na nguo za wanawake kwa asilimia 0.3, sare za shule (asilimia 0.4), viatu vya wanaume (asilimia 0.5), kuni (asilimia 2.3), mkaa (asilimia 1.6), karo za shule (asilimia 0.4) na huduma ya malazi kwenye hoteli na nyumba za kulala wageni kwa asilimia 2.1.
Latest