Matokeo darasa la saba yatangazwa, ufaulu ukiongezeka kwa asilimia 1.2
- Umeongezeka kutoka asilimia 81.5 mwaka 2019 hadi asilimia 82.68 mwaka huu.
- Jumla ya watahiniwa 833,672 kati ya milioni 1.01 waliotunukiwa matokeo wamefaulu.
- Wanafunzi 14,364 hawakufanya mitihani kutokana sababu mbalimbali ikiwemo utoro.
Dar es Salaam. Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA) limetangaza matokeo ya mtihani wa darasa la saba kwa mwaka 2020 huku ufaulu ukiongezeka kidogo kwa asilimia 1.18.
Katibu Mtendaji wa Necta, Dk Charles Msonde aliyekua akitangaza matokeo hayo leo Novemba 21, 2020 Jijini Dar es Salaam amesema watahiniwa 833,672 kati ya milioni 1.01 wamefaulu ikiwa ni sawa na asilimia 82.68.
Ufaulu huo wa mwaka huu upo juu kidogo ikilinganishwa na ufaulu wa mwaka 2019 wa asilimia 81.5.
Dk Msonde amesema kati ya wanafunzi waliofaulu mtihani huo wa elimu ya msingi ni 430,755 ambao ni sawa na asilimia 82.24 na wavulana ni 402,917 sawa na asilimia 83.15. Wanafunzi waliofaulu ni wale waliopata alama 100 na zaidi kati ya alama 250.
Katika mtihani huo watahiniwa milioni 1.02 walisajiliwa kufanya mtihani huo uliofanyika Oktoba mwaka huu wakiwemo wasichana 530,692 sawa na asilimia 51.83.
Soma zaidi:
- NECTA yatangaza matokeo darasa la saba 2020
- Wafahamu wanafunzi 10 bora mtihani darasa la saba mwaka 2020
Dk Msonde amesema watahiniwa milioni 1.01 sawa na asilimia 98.50 ya waliosajiliwa walifanya mtihani huo. Kati yao wasichana walikuwa 524,456.
“Watahiniwa 14,364 sawa na asilimia 1.4 hawakufanya mtihani kutokana na sababu mbalimbali zikiwemo utoro na ugonjwa,” amesema Dk Msonde.
Elimu ya msingi ni kiungo muhimu kwa wanafunzi wanaoendelea na masomo ya sekondari hadi elimu ya juu Tanzania.
Latest
