Watahiniwa 393 wafutiwa matokeo darasa saba, idadi ikipungua
- Ni waliofanya mtihani wa kuhitimu darasa la saba mwaka 2021.
- Idadi hiyo imepungua kutoka 1,059 waliofutiwa mwaka 2020.
- Necta yashauri wachukuliwe hatua kwa vitendo vya udanganyifu wa mitihani.
Dar es Salaam. Watahiniwa 393 waliofanya mtihani wa kuhitimu darasa la saba mwaka 2021 wamefutiwa matokeo yao baada ya kubainika kufanya udanganyifu katika mitihani huo.
Mtihani huo ulifanyika Septemba 8 na 9 mwaka huu na matokeo yake yametangazwa leo jijini Dar es Salaam na Baraza la Mtihani Tanzania (NECTA) na kuonyesha ufaulu wa jumla wa wanafunzi umefikia asilimia 81.97.
Katibu Mtendaji wa NECTA, Dk Charles Msonde amewaambia wanahabari kuwa wamebaini vitendo vya udanganyifu katika mtihani huo uliofanyika na wamechukua hatua ya kufuta matokeo ya watahiniwa hao 393.
Dk Charles Msonde amesema baraza limezishauri mamlaka husika kuwachukulia hatua waliohusika na udanganyifu huo ikiwemo kuwafikisha katika vyombo vya sheria.
“Baraza limezishauri mamla kuwachukulia hatua wale wote waliohusika kwa namna moja au nyingine kusababisha kutokea kwa udanganyifu katika mitihani” amesema Dk Msonde.
Hata hivyo, idadi ya watahiniwa waliofutiwa matokeo mwaka huu imepungua kwa asilimia 62.8 kutoka watahiniwa 1,059 waliofutiwa mwaka 2020.
Pia Necta imezuia kutoa matokeo ya watahiniwa 128 ambao waliugua au kupata matatizo na kushindwa kufanya mtihani kwa masomo yote au baadhi ya masomo.
Dk Msonde amesema watahiniwa hao wamepewa fursa nyingine ya kufanya mtihani wa kumaliza elimu ya msingi mwaka 2022 kwa mujibu wa kifungu 32(1) cha kanuni za mitihani.
Latest