Mama Samia kuiwakilisha Tanzania mkutano wa ‘Africa Now Summit’
- Mkutano huo utafanyika kuazia Machi 12-13 mwaka huu katika jiji la Kampala, Uganda ambapo Mama Samia anamwakilisha Rais John Magufuli.
- Mada zote za mkutano huo zitajikita kwenye kuonyesha chachu ya uongozi katika kuleta maendeleo endelevu barani Afrika.
Dar es Salaam. Makamu wa Rais, Samia Suluhu Hassan anaondoka nchini leo kuelekea jijini Kampala, Uganda kushiriki mkutano wa mwaka 2019 wa ‘Africa Now Summit’ unaolenga kujadili mada mbalimbali ikiwemo uongozi unaohitajika kuchochea mabadiliko ya kijamii na uchumi katika bara la Afrika.
Mkutano huo utafanyika kuazia Machi 12-14 mwaka huu ambapo Mama Samia anamwakilisha Rais John Magufuli.
Taarifa ya Ofisi ya Makamu wa Rais iliyotolewa leo (Machi 11, 2019) inaeleza kuwa mkutano huo utafunguliwa na Rais wa Uganda, Yoweri Museveni ambaye ndiye mwenyeji wa mkutano huu ambapo utakuwa na watoa mada mbalimbali akiwemo Mama Samia Suluhu ambaye atatoa mada ya uongozi unaohitajika katika kuchochea mabadiliko ya kijamii na uchumi katika nchi za Afrika.
Soma zaidi:
- Mama Samia atoa maagizo matano kukuza utalii Tanzania
- Mama Samia ataka hatua zichukuliwe kukabiliana na viumbe vamizi
Viongozi wengine watakaotoa mada ni Rais wa Misri ambaye pia ni Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (UA), Abdel Fattah el Sisi; Rais wa Afrika Kusini, Cyril Ramaphosa; Makamu wa Rais wa Kenya, William Ruto na Waziri Mkuu wa Ethiopia, Ahmed Abiy.
Mada zote zitajikita kwenye kuonyesha chachu ya uongozi katika kuleta maendeleo endelevu barani Afrika.
Mkutano huo wa siku mbili utaanza na hotuba kutoka kwa Rais wa Somalia, Mohamed Abdullahi na baadaye kufungwa rasmi na mwenyeji wake Rais Museveni.
Makamu wa Rais ataambatana na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Dk Damas Ndumbaro.
Pia mkutano huo ambao umeandaliwa na kituo cha Uongozi cha Afrika (ASLC) unakusudia kuwakutanisha wadau mbalimbali wa maendeleo zaidi ya 1,000 ambapo majukumu mengine ya mkutano huo yatakuwa kuunda umoja wa biashara wa vijana, ambao ni muhimu kwa ukuaji wa uchumi. Kutengeneza fursa za kushughulikia changamoto za ajira, kutumia ubunifu na teknolojia ili kuTengeneza mstakabali mzuri wa Afrika.
Latest