Rais Samia: Vyombo vya usalama viongeze kasi, juhudi za uokoaji waliofukiwa na kifusi Shinyanga
Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan ameitaka Ofisi ya Waziri Mkuu pamoja na vyombo vya ulinzi na usalama kupeleka misaada ya dharura na kuongeza juhudi za uokoaji kwa wachimbaji wa madini waliofunikwa na kifusi mkoani Shinyanga.
Agizo hilo limekuja mara baada ya mashimo matatu katika mgodi wa Nyandolwa, Kata ya Mwenge, Wilaya ya Shinyanga Vijijini kufunikwa na kifusi baada kutitia yakiwa na wachimbaji 25 ndani yake.
Kwa mujibu wa taarifa ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mboni Mohamed Mhita idadi ya wachimbaji waliokuwa katika mashimo hayo ni 25, ambapo shimo la kwanza lilikuwa na wachimbaji 11, shimo la pili lilikuwa na wachimbaji 8, na shimo la tatu lilikuwa na wachimbaji 6.
Kati ya hao wanne waliokolewa lakini mmoja aliyeokolewa alifariki dunia baadaye.
Aidha, Rais ametoa pole kwa ndugu, jamaa, na Watanzania wote walioguswa na maafa hayo, akisisitiza mshikamano na msaada kwa familia, zilizoathirika.
“Tuendelee kumwomba Mwenyezi Mungu awajalie pona ya haraka majeruhi, na pia awape subra na nguvu ndugu, jamaa na marafiki wa wale wote walioathiriwa na maafa haya,” amesema Rais Samia.
Latest