Rais Samia kuwa mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya uhuru Msumbiji, Komoro
- Ziara hiyo ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kihistoria na kidiplomasia kati ya Tanzania na mataifa jirani.
Dar es Salaam. Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kufanya ziara katika nchi za Msumbiji na Visiwa vya Komoro ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuimarisha ushirikiano wa kihistoria, kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na mataifa hayo.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Juni 11, 2025 jijini Dodoma na Msemaji Mkuu wa Serikali, Gerson Msigwa, Rais Samia amepokea mialiko rasmi kutoka kwa Marais wa nchi hizo ili awe mgeni katika maadhimisho muhimu ya kitaifa, yakiwemo ya miaka 50 ya uhuru wa Msumbiji.
“Ziara hizi zinatokana na jitihada kubwa za Mheshimiwa Rais katika kuimarisha uhusiano kati ya Tanzania na mataifa mbalimbali duniani. Msumbiji ni jirani yetu wa kihistoria na ndugu wa damu, hivyo mwaliko huu ni heshima kubwa kwa taifa letu,” amesema Msigwa.
Ziara ya Rais Samia nchini Msumbiji inakuja siku chache tu baada ya Rais wa nchi hiyo, Daniel Francisco Chapo kufanya ziara ya kwanza rasmi Tanzania tangu achaguliwe kushika wadhifa huo Januari 15, 2025.
Katika ziara hiyo, viongozi hao walishuhudia utiaji saini wa mikataba miwili na hati nne za makubaliano katika maeneo mbalimbali ya ushirikiano ikiwemo biashara, elimu, utamaduni na huduma za kijamii.
Aidha, Rais Samia pia amepokea mwaliko kutoka kwa Rais wa Komoro Azali Assoumani kushiriki maadhimisho ya miaka 50 ya uhuru wa Muungano wa visiwa hivyo yatakayofanyika Julai 6 mwaka huu.
“Tanzania na Komoro, kama ilivyo kwa Msumbiji ni mataifa ya ndugu yaliyounganishwa na historia ya ukombozi wa Afrika na udugu wa muda mrefu. Ziara hii inalenga kudumisha mshikamano na kukuza fursa za kiuchumi, kiutamaduni na kijamii kwa manufaa ya wananchi wetu,” ameeleza Msigwa.
Latest



