Mahakama yamuachia huru Kabendera, atoa neno
Mwandishi wa habari Erick Kabendera akiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu baada ya kuachiwa huru. Picha|Nuzulack Dausen.
- Mahakama hiyo ilimtia hatiani Kabendera kwa kwa makosa mawili ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha baada ya mshtakiwa kukiri makosa.
- Ameachiwa huru baada ya kulipa faini ya 100,250,000 huku akiwashukuru wote waliokuwa pamoja naye katika kipindi kigumu akiwa jela.
- Mahakama imesema Kabendera hana uwezo wa kukata rufaa kupinga hukumu hiyo.
Dar es Salaam. Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imemuachia huru mwandishi wa habari Erick Kabendera baada ya kulipa faini ya 100,250,000 huku akiwashukuru wote waliokuwa pamoja naye katika kipindi kigumu akiwa jela.
Sambamba na hilo, mwandishi huyo anatakiwa kulipa fidia ya Sh173.24 milioni ndani ya miezi sita tangu hukumu hiyo ilipotewa leo Februari 24, 2020 kutokana na kukwepa kodi.
Hiyo ina maana kuwa atatakiwa kulipa takriban Sh29 milioni kila mwezi ili akamilishe kulipa fidia hiyo.
Uamuzi huo ulitolewa na Hakimu Mkazi Mkuu, Janeth Mtega ambaye amesema Kabendera hana uwezo wa kukata rufaa kupinga hukumu hiyo.
Mapema leo mahakama hiyo ilimtia hatiani Kabendera kwa kwa makosa mawili ya uhujumu uchumi na utakatishaji fedha baada ya mshtakiwa kukiri makosa.
Baada ya Hakimu huyo kueleza hayo, upande wa mashtaka ulimwomba hakimu huyo kutoa hukumu kadri itakavyoona inafaa ila kwa kuzingatia makubaliano kwa kuwa Kabendera ni mkosaji wa mara ya kwanza na hakuna rekodi ya makosa mengine.
Wakili wa Kabendera, Jebra Kambole alimwomba hakimu kuzingatia kuwa mshtakiwa ana familia na ndugu wanaomtegemea.
“Ni zaidi ya miezi sita yupo ndani hili nalo Hakimu lizingatie unapotoa hukumu. Lakini pia mshtakiwa afya yake siyo nzuri,” amesema Kambole.
“Kutokana na mtuhumiwa kukiri makosa yake, namhukumu kama ifuatavyo:
Katika kosa la kwanza kukwepa kodi kulipa faini isiyozidi Sh250,000 au kifungo cha miezi mitatu iwapo atashindwa kulipa faini. Pia, anatakiwa kulipa fidia ya Sh173.25 milioni na kosa la pili la utakatishaji fedha anatakiwa kulipa faini ya Sh100 milioni. Adhabu zote zitakwenda tofauti,” amesema Mtega.
Soma zaidi:
- Polisi Tanznaia yakiri kumshikilia Mwanahabari Kabendera
- Uhamiaji waeleza sababu za kuendelea kumshikilia Mwanahabari Kabendera
- Mwanahabari Erick Kabendera ashitakiwa kwa utakatishaji fedha, uhujumu uchumi
Kabendera aliingia makubaliano na Mwendesha Mashtaka Mkuu wa Serikali (DPP) kukiri makosa yake ambapo upande wa mashtaka umeondoa kosa la kwanza la kuongoza genge la uhalifu.
Kabendera ambaye anaandikia vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi alishtakiwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar es Salaam Agosti 5, 2019 kwa makosa matatu ya uhujumu uchumi, ukwepaji kodi na utakatishaji fedha.
Hata hivyo, mwanahabari huyo ambaye amekaa mahabusu kwa takriban miezi saba amefanikiwa kulipa faini ya Sh250,000 na Sh100 milioni leo, Wakili Kambole amewaambia wanahabari leo baada ya mteja wake kutoka.
Akizungumza nje ya mahakama baada ya kuachiwa, Kabendera amewashukuru wanahabari, ndugu na marafiki ambao walikuwa naye bega kwa bega katika kipindi kigumu alichopitia wakati akiwa jela.
“Binafsi napenda niwashukuru wanataaluma wenzangu kwa kusimama na mimi katika maombi, katika faraja, wengi wenu mmefika kunisalimia hapo Segerea (gerezani) na mmeniletea vitabu vya kusoma, mmeniletea magazeti na mmenitia moyo kusimama katika hali niliyokuwa nayo. Kwa hiyo napenda kuwashukuru sana,” amesema Kabendera mbele ya wanahabari.
#NuktaHanbari
pic.twitter.com/IpEyIjPdfs
— Nukta Tanzania (@NuktaTanzania) February 24, 2020
Latest
