Mahakama Tanzania kusimamia mashauri kielekitroniki

October 16, 2023 8:49 am · Lucy Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni mfumo utaowezesha utoaji wa haraka wa huduma za kimahakama kwa wananchi.
  • Ni miongoni mwa mapendekezo ya Tume ya Haki Jinai yaliyosisitizwa na Rais Samia.

Dar es Salaam. Huenda shughuli za kimahakama zikaimarika zaidi na kuchochea kasi ya upatikanaji wa haki mara baada ya Mahakama ya Tanzania kutangaza kuanza matumizi ya mfumo mpya wa usimamizi mashauri kwa njia ya kielektroniki.

Mfumo huo mpya unaoitwa  ‘E-Case Management System’ unatarajiwa kurahisisha usajili wa mashauri kwa njia ya mtandao, upangaji wa mashauri kwa Majaji na Mahakimu, na kuruhusu mienendo ya mashauri kuandikwa moja kwa moja kwenye mfumo na kuhifadhi kielektroniki.

Taarifa ya Msajili Mkuu wa Mahakama iliyotolewa na Msajili wa Mahakama ya Rufani Sylvester Kainda, leo Oktoba 16, 2023 imebainisha kuwa  mfumo huo ni sehemu ya maboresho yaliyofanyika ili kuimarisha upatikanaji wa haki nchini.


Soma zaidi:Nini hatma ya wakazi wa mikoa 10 maskini zaidi Tanzania?


“Kuanza kwa mfumo huo ni sehemu maboresho yanayofanywa na Mahakama ya Tanzania katika maeneo mbalimbali lengo likiwa ni kuboresha huduma za upatikanaji wa haki kwa wakati na kwa gharama nafuu kwa wananchi,” amesema Kainda.

Taarifa hiyo ya mahakama inakuja ikiwa imepita miezi mitatu tangu Rais Samia alipotoa agizo kwa taasisi za haki jinai kufanya maboresho ya mifumo ya utendaji ambayo haihitaji fedha ili kuimarisha upatikanaji wa haki kwa wananchi.

Awali baadhi ya mifumo iliyokuwepo katika Mahakama ya Tanzania ilikua ikilalamikiwa kutokuwa na ufanisi ukiwemo mfumo wa Mfumo wa Kusajili na kuratibu mashauri kwa njia ya Kieletroniki (JSDS) ulioanza kutumika tangu mwaka 2018.

Ni zaidi ya mfumo

Katika mfumo mpya wa (E-Case ), watumaji wake wataweza kufanya shughuli nyingine zinazotolewa na mifumo mingine kama Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA), na Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), zinazotumika na watanzania wengi.

“Mfumo huo unaweza kusomana na mifumo mingine ya ndani ya Mahakama na ile ya wadau wetu muhimu kama Ofisi ya Taifa ya Mashtaka (NPS), Nida, Rita, na taasisi zingine,” imesema taarifa ya Kainda.

Aidha, mfumo huo utapunguza gharama za usikilizaji wa mashauri kwa upande wa mahamama na wananchi, utapunguza muda wa kusikiliza mashauri na kusogeza zaidi huduma za kimahakama karibu na wananchi.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW