Jeshi la Polisi latoa onyo likiimarisha ulinzi sikukuu za mwisho wa mwaka

December 24, 2021 5:55 am · Mariam John
Share
Tweet
Copy Link
  • Lawataka wazazi kuwalinda watoto wao.
  • Madereva waonywa ulevi na mwendokasi.
  • Waumini wa dini ya Kikristo wahakikishiwa ulinzi. 

Mwanza. Jeshi la Polisi mkoani Mwanza limewakumbusha wazazi na walezi kuwa pamoja na kusherekea sikukuu ya Krismasi na mwaka mpya, wasisahau majukumu yao ya kuwalinda watoto ili kuwaepusha na hatari inayoweza kuwapata.

Wametakiwa kuwa makini na watoto wao kwa kutowaacha peke yao barabarani na katika sehemu za michezo. 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mwanza,  Ramadhan Ng’anzi amesema zipo tabia za wazazi za kuwaacha watoto peke yao kwenye  maeneo ya mialo na michezoni, kitendo ambacho ni hatari. 

Kamanda huyo pia amepiga marufuku  madereva wa vyombo vya moto kuendesha wakiwa wamelewa au mwendo kasi, endapo ikibainika hatua stahiki za kisheria zitachukuliwa dhidi yao. 

“Jeshi la polisi halitaacha kufuatilia,  tutawakamata madereva wote watakaokiuka sheria za usalama barabarani lakini pia na wale  wenye tabia za kuchoma matairi barabarani waache kwani ni kosa kisheria, ” amesema Ng’anzi.

Amesema katika kuhakikisha uhalifu wa aina zote unadhibitiwa, askari watakua wanapita katika maeneo mbalimbali wakiwa kwenye doria za miguu, pikipiki na magari huku wakiwa na mbwa wa Polisi na kuwataka  wananchi wanapowaona watoe ushirikiano kwa askari kwa kuwapa taarifa  za uhalifu au taarifa zozote zenye viashiria vya uhalifu ili uweze kudhibitiwa mapema kabla haujatendeka. 

“Tuwatoe hofu wananchi na wageni wanaotembelea mkoa huu kwamba ulinzi umeimarishwa kwa wao na mali zao,” amesema Ng’anzi.


Zinazohusiana:


Sambamba na hilo Jeshi la Polisi  limewatoa hofu wananchi na wageni wanaotembelea Mkoa huo  kwamba ulinzi umeimarishwa kwa wao na mali zao.

Pia wanachi wanaokwenda kwenye mkesha wa sikukuu za Krismasi na mwaka mpya kutoacha nyumba zao bila uangalizi wa walinzi kwani kunaweza kushawishi wezi kuiba. 

Krismasi kote duniani huwa msimu wa sherehe, kula vinono, mapambo, kuvalia mavazi mapya na ya kupendeza, kujumuika na marafiki, kuwatembelea marafiki, kuwajulia hali wazazi, kwenda likizoni, kufurahia namna mbalimbali.

Kila mtu huisherehekea siku hii kwa mtazamo wake mwenyewe.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW