Jeshi la Polisi lamtaka Polepole kuwasilisha ushahidi wa tuhuma anazotoa
- Ni kwa kuwa zinaashiria uwepo wa makosa ya kijinai hivyo zinatakiwa kuthibitishwa iwapo zitafikishwa mahakamani.
Dar es Salaam. Jeshi la Polisi Tanzania limemtaka aliyekuwa Balozi wa Tanzania Cuba kuwasilisha ushahidi wa tuhuma mbalimbali anazozitoa kwa kuwa zinaashiria uwepo wa makosa ya kijinai hivyo zinatakiwa kuthibitishwa iwapo zitafikishwa mahakamani.
Taarifa iliyotolewa na Msemaji wa Jeshi la Polisi David Misime leo Septemba 15, imebainisha kuwa tayari jeshi hilo lilishafungua jalada la uchunguzi na linaendelea kuchunguza tuhuma mbalimbali ambazo Polepole amekuwa akizitoa tangu Julai 2025.
Kwa mujibu wa Misime, Polepole amekuwa akizitoa tuhuma hizo kupitia mitandao ya kijamii ambapo Jeshi la Polisi baada ya kufungua jalada, kuanza uchunguzi na kukusanya ushahidi limekuwa likifanya jitihada za kumpata ili atoe vielelezo vitakavyothibitisha tuhuma hizo kwa ajili ya hatua zaidi za kisheria.
“Hivyo Jeshi la Polisi kupitia taarifa hii linaendelea kumwelekeza afike katika Ofisi ya Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai ili aweze kutoa maelezo/ushahidi kuhusiana na tuhuma ambazo amekuwa akizitoa kwa umma kupitia Mitandao ya Kijamii,” inasomeka taarifa ya Misime.
Itakumbukwa kuwa Polepole aliandika barua yake ya kujiuzulu Ubalozi wa Cuba Julai 13, 2025 kwenda kwa Rais Samia akitaja sababu ni kutoridhishwa na mwelekeo wa uongozi usiojielekeza katika kusimamia haki, amani na kuheshimu watu.
Hata hivyo, Agosti 5 mwaka huu Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, kupitia kwa Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Balozi Dk Samwel Shelukindo imeeleza imepokea barua kutoka kwa Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Dk Moses Kusiluka ikitaarifu kwamba, Rais Samia Suluhu Hassan kwa mamlaka aliyonayo, ametengua uteuzi wa Humphrey Polepole, aliyekuwa Balozi wa Tanzania nchini Cuba na kumuondolea hadhi ya ubalozi.
Kwa mujibu wa barua hiyo, uamuzi huo umeanza tangu Julai 16, 2025.
Latest
