Idadi ya watalii yashuka miezi miwili mfululizo

November 15, 2022 12:01 pm · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link


  • Imeshuka hadi watalii 133,998 Septemba 2022.
  • Watalii walioingia nchini mwaka huu kuvunja rekodi.

Dar es Salaam. Idadi ya watalii walioingia Tanzania imeshuka mfululizo kwa miezi hadi kufikia 133,998 Septemba mwaka huu huku nchi jirani ya Kenya ikiongoza kuingiza watalii wengi nchini. 

Kwa mujibu wa takwimu za Ofisi ya Taifa ya Takwimu za Septemba 2022 (High Frequency Data) idadi ya watalii hao walioingia Septemba imepungua kutoka watalii 158,049 waliorekodiwa Agosti mwaka huu.

Upungufu huo ni sawa na watalii 24,051 ndani ya kipindi cha mwezi mmoja. 

Idadi ya watalii ilianza kupungua Julai mwaka huu baada ya kushuhudia ongezeko kwa miezi miwili mfululizo. Juni mwaka huu, Tanzania ilipokea watalii 117,349 na mwezi uliofuata waliongezeka hadi 166,736 kabla hawajaanza kushuka miezi iliyofuata. 

Licha ya kuwa idadi ya watalii imekuwa ikipanda na kushuka tangu Januari, huenda mwaka 2022 utarekodi idadi kubwa ya watalii katika kipindi cha miaka miwili iliyopita baada kutoka katika athari za janga la Corona (Uviko-19). 

Mwaka 2020, Tanzania ilipokea watalii 620,867 lakini mwaka uliofuata wakaongezeka hadi 922,692 na huenda wakaongezeka zaidi mwaka huu na kuvunja rekodi.

NBS inaeleza kuwa hadi kufikia Septemba, watalii milioni 1.03 walikuwa wametembelea vivutio mbalimbali nchini tangu mwaka 2022 uanze. 

Idadi hiyo iko juu ikilinganishwa na miaka miwili iliyopita huku nchi za Kenya, Burundi na Marekani zikiongoza kuingiza watalii wengi zaidi. 

Miezi tisa iliyopita, Kenya imeingiza watalii 115,269 ikifuatiwa kwa mbali na Burundi (76,340) na Marekani watalii 73,928. 

Shughuli za utalii nchini huusisha wanyamapori, fukwe za mahari na maziwa, uwindaji na upigaji picha na mikutano. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW