Idadi wanaondoka Ngorongoro yazidi kuongezeka

June 23, 2022 11:41 am · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link

Waziri Mkuu Kassim majaliwa akiwaaga wananchi takribani 117 kutoka kaya 27 wanaohama kwa hiari yao wenyewe kutoka katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro kuelekea kijiji cha Msomera, Handeni. Katika Ofisi za Mamlaka ya Hifadhi ya Eneo la Ngorongoro Karatu, Arusha Juni 23, 2022.


  • Katika awamu ya kwanza na ya pili ni kaya 48 zenye watu 233 na mifugo 899.
  • Hao ni wale waliokubali kuhama kwa hiari kupisha shughuli za uhifadhi.
  • Serikali yasema haitawatupa. 

Dar es Salaam. Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amewahakikishia wakazi wanaohama kwa hiari yao kutoka katika eneo la hifadhi ya Ngorongoro kuelekea kijiji cha Msomera, Handeni mkoani Tanga kuwa wataendelea na  shughuli zao ikiwemo ufugaji katika mazingira bora zaidi.

Waziri Mkuu ambaye ameshuhudia wakazi hao takribani 127 kutoka katika kaya 27 wakihama na kuelekea kijiji cha Msomera, amewahakikishia kuwa Serikali itaendelea kuwapa ushirikiano katika kila eneo.

“Ninawaomba msafiri kwa amani kabisa na mioyo yenu ikunjuke. Isikilizeni Serikali yenu inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan. Sasa hivi mko huru, nenda mkakae kwenye nchi yenu kwa uhuru,” amesisitiza leo Juni 23, 2022) wakati akiwaaga wakazi hao wanaohama kwa hiari yao kwenda kupisha shughuli za uhifadhi katika eneo hilo.

Amesema uamuzi walioufanya wa kuhamia Msomera na kupisha shughuli za uhifadhi katika eneo la Ngorongoro ni uamizi sahihi, hivyo ametumia fursa hiyo kuwahakikishia kwamba hakuna shughuli zao zozote zitakazisimama, wataendelea na ufugaji kwa kuwa Msomera kuna eneo kubwa na la kutosha.


Soma zaidi: 


Hii ni awamu ya pili ya wakazi wanaohama katika eneo hilo kuelekea Msomera. 

Mhifadhi Mkuu wa Ngorongoro, Dk Christopher Timbuka amesema awamu ya pili ya zoezi la kuwahamisha wakazi wa eneo la Ngorongoro kwa hiari lilianza Juni 20, 2022, ambapo inahusisha jumla ya kaya 27 zenye watu 127 na mifugo 488. 

Aidha kaya moja kati ya hizo itahamia Karatu.

Dk Timbuka amesema hadi sasa kaya zilizohama kwa hiari katika eneo la Ngorongoro katika awamu ya kwanza na ya pili ni 48 zenye jumla ya watu 233 na mifugo 899. 

Amesema utaratibu wa kuwahamisha umefanyika kwa kufuata hatua mbalimbali ikiwemo kuhakiki idadi ya watu.

Hatua nyingine ni kusainisha vitabu vya fidia vya wakazi wanaohama kwa hiari awamu ya pili, kuhakiki idadi ya mifugo na kuiweka alama ili iweze kusafirishwa pamoja na kuhakiki na kutambua aina za nyumba za wakazi hao kwa ajili ya taratibu za ubomoaji.

Mbali na kupewa nyumba, fidia na shamba kaya zote, Dk Timbuka amesema kaya zote zitapewa magunia mawili ya mahindi kwa kwa kipindi cha miezi mitatu ili waweze kujikimu katika kipindi cha mpito wakati wakijiandaa na msimu wa kilimo.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...

Enable Notifications OK No thanks