Dk Mwinyi ateua mawaziri, wawili watoka ACT-Walendo
- Ni Mwanasheria Mkuu wa ACT Wazalendo Omar Said Shaaban na Nassor Ahmed Mazrui ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho Zanzibar.
- Mwingine ni Dk Saada Mkuya Salum ambaye aliyewahi kuwa Waziri wa Fedha wa Tanzania
- Uteuzi huo unakamilisha Baraza la Mawaziri katika Serikali ya Zanzibar lenye mawaziri 15.
Dar es Salaam. Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi amewateua mawaziri watatu wakiwemo wawili kutoka chama cha ACT-Wazalendo kusimamia wizara tatu visiwani humo.
Dk Saada Mkuya Salum ambaye ni mjumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar na aliyewahi kuwa Waziri wa Fedha wa Tanzania ameteuliwa kuwa Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais.
Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda, ameteuliwa kuiongoza Omar Said Shaaban ambaye ni Mwanasheria Mkuu wa chama cha ACT Wazalendo.
Nassor Ahmed Mazrui ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo Zanzibar ameteuliwa kuwa Waziri wa Afya, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
“Uteuzi huo unaanzia leo tarehe 3 Machi 2021,” imeeleza taarifa ya Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi wa Zanzibar, Mhandisi Zena Said,
Soma zaidi:
- Masoud Othman aapishwa kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar
- Uzazi wa mpango kufanyika kidijitali
- Alichokisema Dk Bashiru baada ya kuteuliwa kuwa Katibu Mkuu Kiongozi
Rais Mwinyi amefanya uteuzi huo kwa mujibu wa vifungu vya 42, 43(1)(2) na 44 vya katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 ambapo wateuliwa hao watatu wanatarajiwa kuapishwa kesho Machi 4.
“Mheshimiwa Rais atamwapisha pia ndugu Salum Yussuf Ali wa Kamishna wa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB) ambaye alieuliwa Februari 10 mwaka huu,” amesem Said katika taarifa hiyo iliyotolewa leo Machi 3, 2021.
Uteuzi huo unakamilisha Baraza la Mawaziri katika Serikali ya Mapinduzi Zanzibar lenye mawaziri 15.
Kuingia kwa Shaaban na Mazrui katika baraza hilo la Mawaziri kunafuatiwa kuteuliwa na Dk mwinyi kuwa wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar Desemba 7, 2020 ambapo aliacha nafasi mbili katika baraza la mawaziri ambazo zilitakiwa kujazwa na wawakilishi kutoka ACT-Wazalendo.
Latest
