Corona: Gazeti la The Standard halijasitisha uchapishaji
- Gazeti hilo limezushiwa kusitisha uchapishaji kutokana na waandishi wake watatu kukutwa na Corona.
- Kampuni inayomiliki gazeti hilo yasisitiza bado inatoa huduma ikiwemo uchapishaji.
Dar es Salaam. Kama ni mfuatiliaji na msomaji mzuri wa gazeti la The Standard la nchini Kenya , huenda umekutana na habari zisizo za kufurahisha juu ya kufungwa kwa gazeti hilo baada ya wafanyakazi wake watatu kukutwa na ugonjwa wa Corona.
Taarifa hiyo inayosambaa kupitia mitandao ya kijamii hasa wa Twitter haina ukweli wowote kwa sababu uongozi wa kampuni hiyo tayari umekanusha madai hayo na shughuli za gazeti hilo kutoa habari zinaendelea kama kawaida.
Uchunguzi uliofanywa na Nukta Fakti umebaini kuwaa taarifa hiyo iliandikwa na kuchapishwa kwenye akaunti ya Twitter ya gazeti hilo ambayo ni feki na isiyotambulika rasmi.
Taarifa hiyo inasema “Standard Newspaper temporarily closes city centre newsroom at I&M building after three reporters tested positive for COVID-19”.
Kwa tafsiri isiyo rasmi ya Kiswahili ni kuwa “Gazeti la The Standard limefunga ofisi zake za uchapishaji zinazopatikana jengo la I&M kwa muda baada ya waandishi wake watatu kukutwa na Corona”.
Baada ya taarifa hiyo kusambaa mitandaoni, kampuni hiyo imetoa taarifa kukanusha madai hayo na imesisitiza kuwa hayana ukweli wowote na bado uchapishaji unaendelea kama kawaida.
Fake news alert!
Kindly disregard this information saying @Standardkenya I&M office is closed due to covid19#GetTheWholeStory
pic.twitter.com/sUgLEcCWoC— KTN News (@KTNNewsKE) March 27, 2021
“Uzushi! Tafadhali puuza taarifa zinazosambaa kuwa gazeti la Standard Kenya limefunga kwa sababu ya Corona,” inaeleza taarifa ya kampuni hiyo iliyotolewa Jumamosi ya Machi 27, 2021.
Gazeti hilo maarufu Afrika Mashariki linamilikiwa na kampuni ya Standard Group ya nchini Kenya.
Kwa sasa, kampuni hiyo ina bidhaa zaidi ya 12 zikiwemo televisheni ya mtandaoni, KTN News na redio Maisha.
Latest