Cint: Serikali isibague sanaa, wasanii wa vijijini

January 31, 2023 2:03 pm · admin
Share
Tweet
Copy Link
  • Yaishauri Serikali kutoa fursa sawa kwa aina zote za sanaa na wasanii.
  • Wasanii wa vijijini wapate fursa sawa na waliopo mjini.

Dar es Salaam. Wadau wa sanaa Tanzania wameishauri Serikali kutoa kipaumbele sawa kwa aina zote za sanaa na kuachana na utaratibu wa sasa ambao hauwapi kipaumbele wasanii waishio pembezoni mwa miji.

Robert Mwampembwa ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Tasnia ya Ubunifu Tanzania (Cint), aliyekuwa akizindua ripoti ya Mapitio ya Sekta ya Sanaa nchini Tanzania mwaka 2022 amewaambia wanahabari  kuwa hakuna kanuni za kulinda sanaa na ubunifu wa jadi  licha ya kupita miaka 23 tangu  kutungwa kwa sheria inayolinda sanaa za asili.

“Serikali iangalie sanaa na wasanii wote kwani wasanii wa vijijini wamesahaulika, miradi mingi na mipango ya Serikali inawalenga wasanii wa mijini pekee, Serikali ina wajibu wa kuendeleza sanaa zote na isichague baadhi ya sanaa, “ amesema Mwampembwa.

Kwa mujibu wa Mwampembwa Serikali imekua ikitoa zaidi kipaumbele kwa sanaa ya muziki na maigizo pekee na kuacha sanaa nyingine kama uchoraji, ususi au ufumaji ambazo zinahitaji uwezeshaji wa Serikali.


Soma zaidi


Ripoti hiyo pia imebaini pamoja na jitihada za Serikali kutenga fedha kwa ajili ya mfuko wa Utamaduni na Sanaa, imedai kuwa bado mfuko huo unaendeshwa bila utaratibu mzuri kwani unabagua baadhi ya wasanii.

Itakumbukwa Novemba 22, mwaka 2021, Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo pamoja na mambo mengine ilizindua Bodi ya Mfuko wa Utamaduni na Sanaa ambao  awali uliitwa Mfuko wa Utamaduni Tanzania na ulikufa baadaye.

Kwa mujibu wa Innocent Bashungwa ambaye alikuwa Waziri wa Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa wakati huo, mfuko huo umetokana na dhamira ya Rais Samia Suluhu Hassan kukuza sekta ya sanaa ambao utasaidia wasanii kuboresha mawazo, miradi na ubunifu wao.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW