Mambo yatakayosaidia wasanii, wabunifu kuongeza kipato Tanzania
- Ni kwa kuheshimu muda wa kazi na wateja.
- Wasanii wanashauriwa kufanya utafiti kujua bei za masoko.
- Kuongeza ubora, thamani ya kazi zao.
Dar es Salaam. Wadau wa sanaa wameshauri wasanii na wabunifu kutumia kazi zao kama chanzo cha kipato kwa ajili ya kujikimu kimaisha kwa sababu ni sawa na fani nyingine za ajira.
Wadu hao waliokutana leo (Jumamosi Machi12, 2022) katika mkutano wa wasanii ulioandaliwa na jukwaa la Dar Shappers wamesema yapo mambo ambayo wasanii wanaweza kuzingatia ili kuifanya sanaa yao kuwa ajira ikiwemo nidhamu ya muda pamoja na kuwa na maarifa ya tasnia hiyo.
Kuwa na nidhamu na muda
Wasanii wengi wanakwama kutengeneza fedha kwa sababu wanakosa nidhamu ya muda huku kisingizio cha wengi kikiwa ni mtaji pamoja na kukosa muda kutokana na majukumu ama ajira.
Baadhi washindwa kuishi vipaji vyao kwa kuwa wanatumia muda mwingi katika kazi walizosomea ambazo kiuhalisia, zinachukua saa nane tu za siku nzima.
Mbunifu na mtambuzi wa biashara kutoka kituo atamizi cha Smart Lab, Dickson Saurere amesema binadamu yeyote ana saa 24 kwa siku na kinachowatofautisha watu ni namna wanavyogawa saa hizo.
Amesema, kwa mtu aliyeajiliwa, ana saa nane za kazi na saa 16 zinabaki na hivyo anaweza kuzifanyia maamuzi.
“Ukitumia saa sita kwa kulala na kupumzika, unabaki na saa 10. Toa saa tuseme tano za usafiri unabaki na nane. Unazifanyia nini?,” amehoji Saurere.
Kwa wabunifu ambao tayari wapo kwenye ajira, wana uwezo wa kutumia muda huo uliobaki kwa ajili ya sanaa yao na ikawalipa.
Tasnia ya ubunifu ipo katika kila sekta hivyo wabunifu wamehimizwa kuijua thamani yao. Picha| Rodgers George.
Ifahamu thamani yako
Huenda siyo jambo geni kuuliza bei ya kuchorewa picha kwa mtu na akakuambia ni Sh50,000 kwa wakati huo huo, huduma hiyo kwa wengine huenda ikawa ni hadi Sh500,000 na zaidi.
Kwa kuzingatia utofauti huo, unaweza kukufanya uhoji thamani ya msanii na sanaa anayoiweka sokoni.
Mkuu wa Idara ya ubunifu kutoka kampuni ya Smart Codes, Christopher Shayo amesema msanii kuuza bidhaa yake kwa bei ndogo inaashiria kuwa hana ufahamu na uelewa wa thamani ya bidhaa yake sokoni na nguvu aliyonayo juu ya sanaa yake.
Mdau huyo ametolea mfano takwimu zilizotolewa na tovuti ya takwimu ya Statista ambazo zinaonyesha kuwa, zaidi ya Sh177 bilioni zimetumika katika matangazo nchini tanzania kwa mwaka 2021.
Matangazo hayo yalihusisha kazi za sanaa zilizotumika redioni, kwenye televisheni na hata kwenye mabango.
“Kama kampuni inatumia mabilioni kutangaza kazi uliyoitengeneza, kwanini ukubali kulipwa kidogo kwa kutengeneza kazi hiyo?,” amehoji Shayo.
Shayo amesisitiza kuwa ni muhimu wasanii kufahamu thamani ya kazi yao katika sekta zote.
Elimu kwa Watanzania
Jambo linalorudisha nyuma tasnia ya sanaa kwa Watanzania ni pamoja na kukosa elimu juu ya thamani ya sanaa.
Mbunifu na mwana sanaa anayejitegemea, Evon Evance amesema kumwambia Mtanzania kuwa unatengeneza logo (nembo ya biashara) kwa Sh300,000 atakushangaa na kusema “kilogo tu ndiyo bei hiyo?”.
Kwa wakati huo, ukipata mteja wa kimataifa na kumwambia unatengeneza logo hiyo hiyo kwa dola 700 (Sh 1.6 milioni) atahoji kama uko makini na kazi yako kwani ni pesa ndogo sana.
“Watanzania bado hawajaijua thamani ya sanaa hivyo inasababisha kushusha ari ya wasanii kutengeneza pesa kutokana na kazi zao,” amesema Evance anayeshauri Wabunifu kuwaelimisha wateja wao kuhusu thamani ya kazi wanazofanya.
Soma zaidi:
- Vitenge vinapotumika kuongeza nakshi ofisini
- Corona yawaibua wabunifu wa mashine za kunawia mikono Tanzania
- Jinsi ya kukabiliana na mambo yanayozuia wasichana kuwa wabunifu Tanzania
Kuwa na taarifa sahihi
Kukosa taarifa sahihi kunasababisha watu kushindwa kupanga bei sahihi za kazi zao na hivyo kupishana na mpunga wanaostahili.
Mchoraji wa picha za mafuta (acrylic painting), Nias Nyalada amesema baadhi ya wasanii wanakosa fedha kwa sababu hawajui bei za tasnia.
Baadhi wanashindwa kuweka bei zinazoendana na thamani ya kazi zao kwa sababu hawajafanya utafiti au kuongea na waliopo kwenye tasnia husika ambapo pia kufanya kazi zinazofanana kunakosababisha ushindani ambao unashusha thamani ya sanaa.
“Hakikisha unafanya kazi ambayo haiwapi wateja urahisi wa kupata mbadala wako. Fanya kazi ambayo wakikuacha wewe hawatofuata ubunifu wako kwa msanii mwingine,” amesema Nyalada.
Wadau hao wa sanaa wameshauri wasanii kujifua kimaarifa hasa kufahamu mawasiliano chanya ili waweze kuwasiliana vyema na wateja wao pamoja na kuendelea kujisasisha ili wasiachwe na teknolojia kwani wakati ujao unang’aa kwa wasanii.
Saurere amesema wakati mwinginine unakuwa umefanya kazi na makampuni makubwa, watu maarufu lakini kama haujui kuwasiliana vyema, utazikosa hizo kazi.
“Wasanii wajifunze kujibu barua pepe kwa wakati, kuweka bidhaa zao katika majukwaa ya mtandaoni ili iwe rahisi kwa wateja kuwafikia,” amesema Saurere.