Chukua tahadhari: Corona ipo Afrika

August 24, 2021 1:01 pm · TULINAGWE ALSON
Share
Tweet
Copy Link
  • Baadhi ya watu wanaamini Uviko-19 haipo Afrika.
  • WHO yasema ugonjwa huo upo na watu wachukue tahadhari.
  • Pia yaendelea kusisitiza watu kuchanjwa chanjo. 

Dar es Salaam. Kama wewe ni miongoni mwa watu wanaoaminishwa na  uzushi kuwa hakuna ugonjwa wa Corona (Uviko-19) katika nchi za bara la  Afrika, fahamu kuwa umedanganywa na unajiweka katika hatari ya kuathirika na ugonjwa huo usipochukua tahadhari.

Uzushi huo umekuwa ukienezwa hasa kwenye mitandao ya kijamii kuwa ugonjwa huo unawapata watu katika nchi zilizoendelea ikiwemo Ulaya na siyo Afrika.

Kutokana na watu kuamini uzushi huo, hawachukui tahadhari ya kujikinga ikiwemo kuvaa barakoa, kunawa mikono kwa maji tiririka, kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima na kutokutumia vitakasa mikono. 

Pia wengine wameenda mbali zaidi kukataa chanjo ya Uviko-19, jambo ambalo wataalam wa afya wanasema siyo zuri kwa sababu wanapunguza kasi ya kupambana na ugonjwa huo.

Kwa mujibu wa Shirika la Afya Duniani (WHO), Uviko-19 uko Afrika na hadi kufikia Agisti 24, 2021 kumeripotiwa visa milioni 5.5 barani humo huku watu 130,776 wakiripotiwa kufariki katika nchi mbalimbali za bara hilo. 

Pia, WHO inaeleza kuwa nchi 52 kati ya 54 za bara hilo zinatoa chanjo kwa raia wake ikiwa ni nji ya kuwakinga na madhara ya kiafya ya ugonjwa huo.

Nchi ya Burundi na Eritrea ndiyo nchi pekee barani Afrika ambazo hazijaanza kutoa chanjo ya Uviko-19 kwa raia wake.

Licha ya watu kuhimizwa kuvaa kupata chanjo dhidi ya Uviko-19, wametakiwa kuendelea kuchukua tahadhari zote dhidi ya ugonjwa huo ikiwemo kuvaa barakoa, kunawa mikono kwa maji na kuepuka mikusanyiko isiyo ya lazima.

Epuka habari za uzushi kuhusu Uviko-19 kwa kutembelea tovuti za WHO na Wizara ya Afya Tanzania ili kupata taarifa sahihi kuhusu maendeleo ya ugonjwa huo. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW