Afrika yajikongoja utoaji chanjo ya Uviko-19, WHO ikitoa tahadhari
Licha ya dunia kuimarisha mapambano dhidi ya Uviko-19, hadi kufikia Januari 12, watu milioni 312.2 walikuwa wameambukizwa ugonjwa huo huku milioni 5.5 wakifariki dunia kwa maradhi hayo duniani. Picha| Mtandao.
- Afrika yajikongoja utoaji chanjo ya Uviko-19, WHO ikitoa tahadhari.
- Asilimia 85 ya watu wa bara hilo bado hawajapata hata dozi moja ya chanjo ya Uviko-19.
- Shirika la Afya Duniani (WHO) kuongeza dozi bilioni 1 za chanjo kwa siku zijazo.
Dar es Salaam. Shirika la Afya Duniani (WHO) limesema zaidi ya asilimia 85 ya watu wanaoishi barani Afrika bado hawajachanjwa hata dozi moja ya chanjo dhidi ya Corona (Uviko-19) tangu ilipoanza kutolewa mwaka jana, jambo linalorudisha nyuma mapambano ya ugonjwa huo duniani.
Hiyo ni sawa kusema takriban watu wawili barani humo ndiyo wamepata chanjo ya ugonjwa huo.
“Hatuwezi kumaliza janga isipokuwa tukifunga pengo hili,” amesema Mkurugenzi Mkuu wa WHO, Dk Tedros Ghebreyesus katika mkutano na waandishi wa habari Januari 12, 2022 mjini Genva Uswisi alipokuwa akieleza hali ya mapambano dhidi ya Covid-19.
Dk Tedros amesema pamoja na changamoto hizo, WHO inapiga hatua katika mapambano dhidi ya ugonjwa huu kwa mwezi Desemba 2021, COVAX ilisafirisha zaidi ya mara mbili ya idadi ya dozi ilizozisafirisha mwezi Novemba,
“Katika siku zijazo tunategemea COVAX kusafirisha dozi yake ya bilioni 1,” amesema Tedros.
Mkuu huyo wa WHO ameeleza kuwa baadhi ya vikwazo walivyokabiliana navyo mwaka jana vya utoaji wa chanjo hasa barani Afrika vimeanza kupungua.
“Bado tuna safari ndefu kufikia lengo letu la kuchanja asilimia 70 ya watu wa kila nchi ifikapo katikati ya mwaka huu. Nchi 90 bado hazijafikia lengo la asilimia 40, na 36 kati ya nchi hizo zimechanja chini ya asilimia 10 ya watu wao,” amesema Dk Tedros.
Kwa mujibu wa WHO, hadi kufikia Januari 10, 2022 dozi za chanjo ya Corona bilioni 9.2 zilikuwa zimetolewa ambapo watu bilioni 4.6 walikuwa tayari wamechanjwa duniani kote.
Licha ya dunia kuimarisha mapambano dhidi ya Uviko-19, hadi kufikia Januari 12, watu milioni 312.2 walikuwa wameambukizwa ugonjwa huo huku milioni 5.5 wakifariki dunia kwa maradhi hayo duniani.
Soma Zaidi:
Mapambano dhidi ya Omicron kuendelea
Mwezi Septemba mwaka jana, WHO ilianzisha Kundi la Ushauri wa Kiufundi kuhusu Uzalishaji wa Chanjo ya Uviko-19 (TAG-CO-VAC).
Timu hiyo ya wataalamu inaangalia na kukagua athari za minyumbuliko ya ugonjwa HUO katika uzalishaji wa chanjo. Jana, TAG-CO-VAC ilisisitiza hitaji la dharura la ufikiaji mpana wa chanjo zilizopo, na kwamba chanjo zaidi zinahitajika ambazo zina utendaji mkubwa zaidi katika kuzuia maambukizi na uambukizaji.
“Mpaka chanjo kama hizo zitakapotengenezwa, muundo wa chanjo za sasa za uVIKO-19 zinaweza kuhitaji kuboreshwa, ili kuhakikisha kuwa zinaendelea kutoa viwango vilivyopendekezwa na WHO vya ulinzi dhidi ya maambukizo na magonjwa.” imeeleza TAG-CO-VAC.
Pia mkakati wa chanjo wa kutegemea dozi za kurudia rudia mara kwa mara kwa chanjo ile ile hauwezi kuwa endelevu.
Timu hiyo ya wataalamu ilisisitiza kuwa wakati baadhi ya nchi zinapendekeza chanjo ya nyongeza, kipaumbele cha haraka kwa ulimwengu ni kuongeza kasi ya upatikanaji wa chanjo ya msingi, hasa kwa makundi ya watu walioko katika hatari kubwa ya kuambukizwa.
Dkt Tedrs ameeleza kuwa idadi kubwa ya watu wanaolazwa katika hospitali kote ulimwenguni hawajachanjwa na kwamba maambukizi mengi yanamaanisha kulazwa hospitalini zaidi, vifo vingi, watu wengi zaidi kukosa kazi, wakiwemo walimu na wahudumu wa afya.
“Hatari zaidi ya minyumbuliko mingine kuibuka ambayo inaweza kuambukiza na kuua zaidi kuliko Omicron. Idadi kubwa ya maambukizi inamaanisha shinikizo zaidi kwa wafanyakazi wa afya ambao tayari wameelemewa na wamechoka,” amesema Dk Tedros.
Latest