BOT mbioni kupokea sarafu zisizotumika ili kulinda ubora wake
- Ni baada ya kubaainika uwepo wa sarafu nyingi zisizotumika.
- Zitabadilishwa na noti au kuhifadhiwa kama amana.
- Zoezi kudumu kwa mwezi mmoja pekee.
Dar es Salaam. Benki Kuu ya Tanzania (BOT) imetangaza kuwa iko mbioni kuanza kutoa huduma ya kupokea sarafu (coin) zilizotunzwa kwa muda mrefu bila kutumika kwa wananchi wote au taasisi ili kubadilishwa na noti.
Gavana wa BOT Emmanuel Tutuba katika taarifa yake aliyoitoa leo Disemba 29, 2023 amebainisha kuwa huduma hiyo itatolewa katika ofisi zote za BOT pamoja na benki za biashara nchini kuanzia Januari 2, 2024.
— Bank of Tanzania (@BankOfTanzania) December 29, 2023
“Hatua hii imechukuliwa kutokana na utafiti uliobaini kuwepo kwa sarafu nyingi za shilingi 200, 100, na 50 ambazo hazitumiki kwa muda mrefu katika mzunguko wa kiuchumi na badala yake zimetunzwa au kuwekwa nyumbani, ofisini, kwenye magari, biashara na taasisi mbalimbali nchini,” amesema Tutuba.
Tutuba ameongeza kuwa huduma hiyo itatolewa kama zoezi maalumu la mwezi mmoja ili kuendelea kulinda ubora wa sarafu dhidi ya uharibifu unaotokea katika mazingira yasiyokuwa salama na kurejesha fedha hizo kwenye mzunguko wa kiuchumi.
“Hivyo, wananchi wote wenye sarafu za Sh200, 100 na 50 ambazo zimetunzwa bila kutumika kwa muda mrefu na wangependa kuzibadilisha ili kupata noti au kuzitunza kama amana katika akaunti zao, wanaombwa kuziwasilisha kwenye ofisi za BOT au benki za biashara kwa ajili ya kupata huduma hiyo,” amesisitiza Tutuba.
Latest