Bei za mazao makuu ya chakula zang’ang’ania kiwango cha Jumatano
- Mchele na maharage ndiyo mazao yanayouzwa kwa bei ya juu zaidi kuliko mazao mengine ya chakula.
- Bei hizo hazijabadilika tangu Jumatano, Januari 26, 2022.
Dar es Salaam. Bei za jumla za baadhi ya mazao makuu ya chakula ikiwemo mahindi zinazotumika leo katika mikoa mbalimbali Tanzania Bara imeendelea kubaki katika kiwango kile kile kilichorekodiwa jumatano Januari 26, 2022.
Mazao mengine ambayo bei hazijabadilika ni mchele, maharage na viazi mviringo.
Hata hivyo, mchele na maharage ndiyo mazao yanayouzwa kwa bei ya juu zaidi kuliko mazao mengine.
Kwa mujibu wa takwimu za mazao makuu ya chakula zilizotolewa leo (Januari 28, 2022) na Wizara ya Viwanda na Biashara zinaeleza kuwa bei ya juu ya gunia la kilo 100 la mahindi linauzwa kwa Sh100,000 katika mikoa ya Dar es Salaam na Morogoro.
Aidha bei ya gunia la kilo 100 la mchele pamoja na maharage yanauzwa kwa Sh250,000 kila moja ambayo ni bei ya juu kabisa ya zao hilo.
Bei ya juu mchele imerekodiwa katika mikoa ya Njombe, Mwanza na Dar es Salaam huku maharage yakiuzwa kwa bei ya juu katika mikoa ya Mwanza, Lindi na Dar es Salaam.
Wakati bei ya juu ya mazao hayo zikirekodiwa katika mikoa hiyo, bei ya chini ya mahindi ni Sh46,000 mkoani Dodoma, mchele ni Sh150,000 katika mikoa ya Dodoma, Katavi, Kigoma, Morogoro, Mwanza na Kagera.
Wakati huo huo bei ya chini ya gunia la kilo 100 la maharage linauzwa Sh120,000 katika mikoa ya Kagera na Kigoma huku viazi mviringo kwa bei ya chini vikiuzwa kwa Sh46,000 katika mkoa wa Njombe.
Bei hiyo haijabadilika inaendelea kutumika kama ilivyokuwa Jumatano katika mkoa hiyo hiyo.
Ifahamike kuwa utaratibu wa kutoa bei za jumla za mazao makuu ya chakula hufanyika mara tatu kwa wiki yaani Jumatatu, Jumatano na Ijumaa.

Latest