Maoni mseto bei ya mafuta ikishuka miezi mitatu mfululizo Tanzania
- Wananchi wasema punguzo hilo halitakuwa na matokeo yoyote kwa sababu bado nauli na gharama za maisha zipo juu.
Dar es salaam. Saa chache baada ya Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji, (Ewura) kutangaza kushuka kwa bei za mafuta, baadhi ya wamiliki wa vyombo vya moto na abiria wametoa maoni mseto.
Kwa mujibu wa taarifa ya Ewura iliyotolewa leo Septemba 2, 2026 petroli inayopitia Bandari ya Dar es Salaam sasa inauzwa Sh3,796, ikiwa imepungua kwa Sh102 kutoka bei ya Agosti, huku dizeli ikishuka hadi Sh3,877 baada ya kupungua Sh101 kulinganisha na mwezi uliopita.
Kufuatia kushuka kwa bei hiyo baadhi ya wakazi wa Dar es Salaam wamesema punguzo hilo bado halitakuwa na matokeo yoyote kwa sababu nauli na gharama za maisha zipo juu.
“Kiufupi suala la kushuka kwa bei ni zuri lakini hatua inayoshuka ni ndogo sana ukilinganisha na ilivyokuwa imependa hapo mwanzo, kwa sababu unakuta inapanda Sh1,000 lakini ikushuka inashuka Sh70 au Sh100 kwa hiyo tunajikuta maumivu bado yapo pale pale,” amesema Dastani Luiga, afisa usafirishaji (bodaboda) Lumumba.
Naye Mwaka Kastory, afisa usafirishaji Kinondoni Biafra amesema “Tumepokea vizuri lakini bado tuna maumivu kwa sababu yalipanda sana lakini yameshuka kidogo,”

‘Nauli zishuke’
Wakati madereva wa vyombo vya moto wakipata ahueni kiduchu, baadhi ya abiria mkoani Dar es Salaam wamesema baada ya mafuta kushuka wanatamani nauli pia zishuke.
“Punguzo hilo lingeonekana kwenye magari yanayotoka kuchukua bidhaa kutoka shamba kwenda mjini, kwa sababu sisi wananchi tunapata nafuu ya kuchua chakula kutoka shamba kuja mjini”. Selemani Abdillah, mkazi wa kinondoni.
Mbali na nauli kushuka, Ivan Michael mkazi wa Mbezi ameiambia Nukta Habari kuwa anatamani kuona baadhi ya bidhaa muhimu ikiwemo za chakula zikishuka ili kupunguza ukali wa maisha.
“Bidhaa ambazo natamani zishuke bei ni zile za madukani ikwamo maji ya kunywa, mafuta ya kula na mchele ambavyo vimepanda kutokana na mafuta kupanda bei,” amesema Ivan Michael.
Kwa mujibu wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) mfumuko wa bei wa Taifa kwa mwaka ulioishia mwezi Julai, 2026 umeongezeka hadi asilimia 4.2 kutoka asilimia 4.0 kwa mwaka ulioishia mwezi Juni, 2026.
Miongoni mwa huduma zilizopaisha mfumuko huo ni usafiri, vyakula na vinywaji baridi, samani, vifaa vya nyumbani na ukarabati wa makazi.
Mtaalamu wa fedha na uchumi kutoka jijini Dar es Salaam Paul Chengula amesema bei za bidhaa haziwezi kushuka kwa haraka kwa sababu bado baadhi ya wafanyabiashara wanauza bidhaa zilizotengenezwa kwa gharama za zamani.
“Mfanyabiashara ataziuza kwa gharama ile ile kubwa, lakini huko mbeleni baada ya muda kidogo ndiyo zinaweza zikaja ‘zika-adjust’ kwa pamoja,” amesema Chengula.