Mfumuko wa bei Tanzania wapungua kwa 0.2% Juni 2026
- Hii ni baada ya kupaa na kufikia asilimia 4.2 mwezi Mei, kiwango cha juu zaidi kuwahi kurekodiwa ndani ya miaka mitatu.
Dar es Salaam. Kasi ya mfumuko wa bei za huduma na bidhaa nchini Tanzania imeshuka hadi asilimia 4.0 mwezi Juni 2026 baada ya kupaa na kufikia kiwango cha juu zaidi kuwahi kurekodiwa ndani ya miaka mitatu mwezi iliopita.
Hii ina maanisha kuwa bei ya huduma na bidhaa imepungua kwa asilimia 0.2 kutoka asilimia 4.2 iliyorekodiwa Mei mwaka huu, kasi iliyochagizwa zaidi na kuongezeka kwa bei ya mafuta katika soko la dunia.
Kwa mujibu wa takwimu hizo zinazotolewa na Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) huduma ya usafiri ndiyo huduma iliyoongoza kwa kuwa na bei ya juu zaidi ikirekodi asilimia 1.6 mwezi juni.
Mfumuko wa bei ni hali ya kupanda kwa bei za huduma na bidhaa katika uchumi kwa kipindi fulani. Kwa lugha nyepesi, ni hali ambayo fedha ile ile uliyonayo mwananchi inanunua vitu vichache zaidi kulinganisha na awali.
Kufuatia kupungua kwa kasi ya mfumuko huenda Watanzania wakapata ahueni kiduchu mwezi Julai ambapo uwezo wa kununua bidhaa utakuwa mkubwa zaidi kuliko ilivyokuwa mwezi Juni.
Huenda kasi ikashuka zaidi
Uchambuzi uliofanywa na Nukta Habari unabainisha kuwa huenda kasi ya mfumuko wa bei ikaendelea kushuka zaidi baada ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) kuongeza riba ya benki kuu (CBR) hadi asilimia 6.25 katika robo ya tatu ya mwaka 2026 kwa lengo la kudhibiti mfumuko wa bei.
Kuongezeka kwa riba ya BoT kutafanya mikopo katika taasisi za fedha na benki za kibiashara zinazokopa katika benki hiyo kuwa ghali zaidi jambo litakalochagiza kubana matumizi na mzunguko wa fedha kwenye uchumi hivyo kusaidia kushusha shinikizo la kupanda kwa bei.
Aidha, hali hiyo inaweza kuchagizwa zaidi na ahueni ya bei ya mafuta kwenye soko la dunia tangu makubaliano ya kusimama kwa vita Mashariki ya Kati kufanyika baina ya Iran na Marekani.
Huenda ahueni hiyo isiwe ya muda mrefu baada ya Marekani kuanzisha wimbi jipya la mashambulizi ya anga dhidi ya Iran Juai 8 mwaka huu hali inayoibua hofu ya kupaa kwa bei za mafuta katika masoko ya dunia.
Katika mahojiano na Nukta Habari hivi karibuni mchambuzi wa masuala ya uchumi Paul Chengula kutoka mkoani Dar es Salaam aliwataka wananchi kutotegemea hali ya sasa pekee, akieleza kuwa mabadiliko ya bei katika soko la dunia yanaweza kujitokeza tena wakati wowote.
Ameshauri kujenga utamaduni wa kuweka akiba na kuwa na mfuko wa dharura (emergency fund) ili kukabiliana na misukosuko ya kiuchumi isiyotarajiwa.
Maumivu Kenya
Wakati mfumuko wa bei ukipungua nchini Tanzania nchi jirani ya Kenya bado inaendelea kuongoza kwa asilimia 6.4 licha ya kupungua kwa asilimia 0.3 kulinganisha na mwezi uliopita.
Taifa la Uganda ndio lenye kiasi ya chini zaidi ya mfumuko wa bei licha ya kuongezeka kwa asilimia 0.5 na kufikia asilimia 3.7 kutoka asilimia 3.2 mwezi Mei.