Rais Samia: Jitokezeni kuhesabiwa mwakani

September 14, 2021 12:29 pm · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link
  • Amesema sensa ni kwa ajili ya maendeleo.
  • Takwimu zitakazokusanywa zitarahisisha kazi za Serikali.
  • Asema zitasaidia kujua nyumba na makazi na kuongeza wigo wa tozo za majengo.

Dar es Salaam. Rais wa Tanzana Samia Suluhu Hassan amewahimiza Watanzania kuipokea kwa mikono miwili Sensa ya Watu na Makazi inayotarajiwa kufanyika mwak 2022 kwa sababu sensa hiyo  inaambatana na manufaa mengi ikiwemo kukusanya taarifa za kusaidia uwekezaji wa nchi.

Rais Samia ameyasema hayo leo Septemba 14  jijini Dodoma katika uwanja wa Jamhuri wakati wa uzinduzi wa mkakati wa uelemishaji wa sensa uliohudhuriwa na viongozi mbalimbali na wananchi.

Katika kuhamasisha Watanzania kushiriki kikamilifu kwenye sensa hiyo, Mkuu huyo wa nchi amesema sensa ina faida kubwa kwa Taifa ikiwemo uwekezaji lakini zaidi itasaidia maendeleo ya nchi.

“Taarifa za sensa zinatumiwa na Jumuiya za Kimataifa, Sekta Binafsi na Asasi za Kiraia kufanya maamuzi ya kimaendeleo, mfano wafanyabiashara na wawekezaji hutumia taarifa za Sensa kufanya maamuzi ya aina ya biashara na uwekezaji, wawekeze wapi na kwa kiasi gani,” amesema Rais Samia.

Aidha, Mama Samia amesema katika sensa ya mwakani itahusisha kuhesabu nyumba na makazi ya watu zitakazosaidia katika kuboresha maisha ya Watanzania na kuimarisha uwajibikaji.

“Sensa hii itaenda pia kuangalia majengo na anuani za makazi, hili ni jambo zuri sana kwasababu tangu tumepata uhuru hatujawahi kufanya Sensa ya Majengo,” amesema Rais.

Rais Samia amefanya uzinduzi wa mkakati wa uelimishaji na uhamasishaji wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022. Picha Ikulu Tanzania.

Amesema utambuzi wa nyumba  na makazi ya watu utarahishisha zoezi la ukusanyaji wa tozo ya majengo unaofanyika kupitia miamala ya simu na hivyo kuongeza wigo wa Serikali kupata mato na kutoa huduma kwenye jamii.

“Tumeweka tozo ya makazi. Makazi yale kulipiwa kiasi fulani cha fedha lakini hatukuwa na idadi sahihi ya nyumba na makazi ya Watanzania nchini. Kwa hiyo zoezi hili litaenda kutupa ubora huo na kujiamini kwamba tunafanya kazi kwa kujua anuani za makazi na idadi ya majumba na aina za nyumba zilizopo nchini mwetu,” amesema kiongozi huyo mkuu wa nchi.

Mbali na kurahisisha ukusanywaji wa kodi za majengo, takwimu za idadi ya watu na makazi zitasaidia katika kurahisisha mgawanyo wa rasilimali pamoja na ujenzi wa miundombinu.

Endapo Serikali haina hesabu au takwimu sahihi, haiwezi kugawa rasilimali na kutoa huduma kwa haki, uwiano na inavyopaswa zitolewe. 

Pia ukosefu wa takwimu unakwamisha kushughulikiwa kwa changamoto mbalimbali ikiwemo za ajira na jamii.

“Taarifa za sensa zitaiwezesha nchi kutambua hatua mbalimbali za maendeleo mathalan sensa ya mwakani itatusaidia kupima maendeleo yaliyopatikana tangu kufanyika kwa sensa ya mwisho ya mwaka 2012,” amesisitiza Rais Samia.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW