Tanzania mbioni kuuza mazao ya wanyamapori
- Ni mazao yenye uhitaji kwenye jamii ikiwemo ngozi, mikia na kucha.
- Ni njia mojawapo ya kuondosha mazao yasiyo halali.
- Inaandaa utaratibu kutekeleza suala hilo.
Manyara. Serikali ya Tanzania iko mbioni kuanzisha biashara ya mazao ya wanyamapori chini ya uratibu maalum ili kukidhi mahitaji mbalimbali ya jamii ikiwemo shughuli za utamaduni na tiba mbadala.
Hatua hiyo imekuja baada ya kuruhusu uuzaji halali wa nyamapori katika mabucha maalum ambayo inatokana na mashamba yanayofuga wanyama hao na wale wanaopatikana kwa vibali katika maeneo ya hifadhi.
Kwa mujibu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), kuna bucha 34 za nyamapori lakini zinazofanya kazi ni 14 tu.
Kutokana na kuongezeka kwa mahitaji ya mazao ya wanyamapori, Serikali inakusudia kuruhusu uuzaji wa mazao hayo ambayo yatawekewa utaratibu maalum ambao hautaathiri uhifadhi na ekolojia ya wanyamapori nchini.
Baadhi ya mazao yenye uhitaji ni pamoja na mavi ya tembo, mkia wa nyumbu, ngozi, kucha na mafuta ya wanyamapori mbalimbali.
“Serikali inaendelea na mchakato wa kuanzisha utaratibu ambao utawezesha sehemu (viungo) za wanyama ambazo zimepatikana kihalali kwa kufuata taratibu kutokana na yale mahitaji basi zile sehemu za mnyama ziweze kutumika,” amesema Afisa Mhifadhi Mwandamizi wa TAWA, Wibright Munuo.
Baadhi ya nyara za Serikali za faru, viboko ambazo zilikamatwa wakati wa operesheni tokomeza ujangili ambazo zimehifadhiwa katika ofisi ya Halmashauri ya Rufiji. Picha|Daniel Samson.
Amesema pia biashara hiyo itahusisha mazao ya wanyama yaliyokamatwa na Serikali kutokana na vitendo vya uhalifu ikiwemo ujangili ambapo yatauzwa kama njia ya kuyaondosha.
“Kwenye kuondosha unaweza kuondosha; aidha kwa kuteketeza au kwa matumizi. Kama ni ngozi yenye thamani nzuri ile ngozi itauzwa, kama ni mikia au ni pembe za mnyama fulani zina matumizi ina maana zile nyara zitaondoshwa kwa kufuata taratibu,” amesema Munuo.
Munuo alikuwa akiongea na Nukta Habari (www.nukta.co.tz) Desemba 13, 2021 mkoani Manyara kando ya warsha ya wanawahabari kuhusu uhifadhi wa wanyamapori.
Warsha hiyo iliyoandaliwa na shirika lisilokuwa la kiserikali la TRAFFIC kwa ufadhili wa shirika la Maendeleo la Watu wa Marekani (USAID) chini ya mradi wa CONNECT ina lengo la kutoa uelewa juu masuala ya uhifadhi, umuhimu wa watu kuishi vema na viumbe pori.
Pia kujenga na kubadili tabia ya jamii kuhusu wanyamapori na umuhimu wao kwenye maendeleo yao na nchi kwa ujumla.
TRAFFIC ni mtandao wa ufuatiliaji wa biashara ya viumbepori. Tunafuatilia biashara halali na haramu ya viumbe pori.
Soma zaidi
- Zifahamu mbuga za wanyama kubwa zaidi Afrika Mashariki
- Mbuga za wanyama, fukwe vinara kutembelewa na watalii Tanzania
- Wafahamu zaidi wanyama hawa adimu Tanzania
Mwezi uliopita, waandishi wa habari walishiriki kwenye mafunzo yaliyoandaliwa na Journalists Environmental Association of Tanzania (JET) kuhusu uhifadhi wa maliasili, migogoro ya mwingiliano wa binadamu na wanyama pori katika shoroba, yakiwa na lengo kubwa la kuongeza uelewa wao ili waweze kutumia taaluma yao kuhabarisha wananchi na wadau mbalimbali.
Kwa sasa, Serikali iko katika mchakato wa kuangalia namna gani itatekeleza suala hilo kwa ufanisi ili kukidhi mahitaji ya wananchi bila kuathiri shughuli za uhifadhi.
Kwa mujibu wa Munuo, tathmini ya mahitaji hayo inafanyika kwa kukutana na wadau mbalimbali wakiwemo wataalam wa tiba mbadala na wanaohusika na masuala ya mila na utamaduni ili kupata maoni na njia nzuri ya kuwahudumia.
Sambamba na hilo, Serikali itaanzisha ghala maalum la kutunza mazao hayo na kisha kuyapeleka soko inapohitajika.
Huenda hatua hiyo itasaidia Serikali kupata mapato kutokana na viungo vya wanyamapori huku ikizifaidisha jamii ambazo zimekuwa zikihitaji mazao hayo lakini zinakosa utaratibu wa kuyapata.
Pia itasaidia kupunguza ujangili na biashara haramu ya wanyamapori ambayo imekuwa ikitishia uhifadhi endelevu wa wanyama hao.
Latest