Majaliwa: Tutawadhibiti wanyamapori, wananchi waishi kwa amani
- Ni baada ya wanyamapori wakiwemo tembo kuvamia makazi ya watu
- Mifumo kuimarishwa kuzuia wanyama hao kufanya uharibifu.
- Vituo 32 vya kuhifadhia silaha kujengwa kando kando na hifadhi za wanyamapori.
Dar es Salaam. Huenda migogoro ya binadamu na wanyamapori ikapungua Tanzania, baada ya kuimarishwa kwa mifumo ya kuwadhibiti wanyama hao wasiingie kwenye makazi ya watu na kufanya uharibifu wa mali yakiwemo mashamba.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amesema Serikali inaendelea kuimarisha mifumo hiyo ambayo itazuia wanyamapori wakiwemo tembo kuingia katika makazi ya watu.
Majaliwa ameliambia Bunge jijini Dodoma leo (Juni 9, 2022) kuwa kutokana na juhudi za Serikali kuimarisha ulinzi na kuzuia uwindaji haramu wanyama wengi wameongezeka hivyo inaendelea kuwadhibiti wasiingie kwenye makazi ya watu.
“Tutaimarisha ulinzi ili kuzuia wanyamapori kuingia kwenye makazi ya wananchi na kuhakikisha madhara hayo hayajitokezi tena. Tutaendelea kudhibiti maeneo hayo ili wananchi waishi kwa amani.” amesema Majaliwa.
Wizara ya Maliasili na Utalii inaratibu ujenzi wa vituo 32 vya kuhifadhia silaha kando kando ya maeneo yanayopakana na hifadhi za wanyamapori.
Waziri Mkuu Majaliwa amesema lengo la Serikali ni kuendeleza uhifadhi wa wanyamapori hao na kuwahakikishia wananchi wanaoishi maeneo ya pembezoni mwa usalama wao.
Majaliwa alikuwa akijibu swali la Mbunge wa Mlalo Rashidi Shangazi aliyetaka kujua Serikali inafanya nini kuwalinda wananchi wanaoishi pembezoni mwa hifadhi wasiendelee kupata athari zinazosababishwa uvamizi wa wanyamapori