Jafo: Takwimu za hali hewa zitumike katika tathmini za mazingira
- Aagiza miradi inayoanzishwa kutumia takwimu za hali ya hewa.
- Hayo ni matakwa ya Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania ya 2019.
Dar es Salaam. Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Selemani Jafo amewaagiza wadau wa mazingira kutumia takwimu sahihi za hali ya hewa katika kuandaa tathmini za athari kwa mazingira nchini.
Amesema hatua hiyo ni kutekeleza matakwa ya sheria namba 2 ya mwaka 2019 ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania.
Jafo ametoa maelekezo hayo wakati akifungua rasmi warsha ya wadau wa mazingira kuhusu umuhimu wa huduma za hali ya hewa, iliyofanyika katika Ukumbi wa Maktaba, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), jana Februari 18, 2022.
“Nikiwa waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) nitahakikisha kabla ya kutoa vyeti tathmini za athari kwa mazingira (EIA), jambo kubwa nitakaloliangalia ni chanzo cha takwimu zilizoambatanishwa, hivyo hakuna namna ya kukwepa, tutumie takwimu sahihi za hali ya hewa kwa mustakabali wa nchi yetu,” amesema Jafo.
Amesema kila mradi unaotaka kuwekezwa unatakiwa kufanyiwa tathmini za athari za mazingira, na mchakato wa EIA ni lazima unahitaji takwimu za hali ya hewa, na ikitokea umekosea takwimu utaleta shida.
Aidha, Jafo ameeleza kuwa Sheria ya Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania inaipa mamlaka hiyo jukumu la kutoa takwimu za hali ya hewa na kuzitaka wizara, taasisi na wataalam elekezi wa mazingira kuzingatia umuhimu wa matumizi ya takwimu za hali ya hewa na endapo takwimu hizo zitakosekana inatakiwa kupata ushauri wa kitaalamu kutoka TMA na kutokufanya hivyo ni kuvunja sheria za nchi.
Soma zaidi:
- TMA yatahadharisha ujio mvua kubwa
- Watanzania washauriwa kutumia taarifa za hali ya hewa kwenye mipango ya maendeleo
- Ujio mfumo wa taifa wa hali ya hewa kuchochea ujenzi wa viwanda nchini
Vilevile, Jafo ameitaka TMA kuandaa semina kwa maafisa mazingira waliopo katika halmashauri na mikoa yote nchini ili wafahamu vyema masuala muhimu ya hali ya hewa kama ilivyoainishwa katika sheria.
Pia kutoa mada kwenye vikao vya wakurugenzi wa jiji na halmashauri, ili kuwajengea uelewa wa sheria hiyo.
Mkurugenzi Mkuu wa TMA, Dk Agnes Kijazi amesema kuwa warsha hiyo ni fursa muhimu ya kuboresha huduma katika sekta ya mazingira kwa kuzingatia matumizi sahihi ya huduma za hali ya hewa zinazotolewa na TMA na matakwa ya kisheria pamoja na kuimarisha uelewa kuhusiana na changamoto za mabadiliko ya hali ya hewa na tabianchi.
Aidha, Dk Kijazi ambaye ni Makamu wa tatu wa Rais wa Shirika la Hali ya Hewa Duniani (WMO) amewajulisha washiriki wa warsha hiyo kuwa huduma za hali ya hewa zinazotolewa nchini zimeongezeka viwango vya usahihi hivyo zinafaa kutumika katika sekta zote za maendeleo.
Latest