Zaidi ya bilioni 3.8 kutumika uapisho wa Rais mteule Kenya
- Zitatumika kuandaa sherehe ya uapisho na kukabidhi madaraka.
- Pia kurahisisha mawasiliano ya Rais anayemaliza muda wake na Rais mpya.
- Pia kuandaa ulinzi, vifaa na wafanyakazi wa Rais mpya.
Dar es Salaam. Wizara ya Fedha ya Kenya kupitia hazina imetenga kiasi Sh 3.8 bilioni kwa ajili ya shughuli ya uapisho wa Rais mteule, William Ruto itakayofanyika wiki ijayo.
Pia kiasi hicho cha fedha kitatumika katika shughuli nyingine ya kukabidhi mamlaka kutoka kwa Rais wa sasa ambaye anamaliza muda wake, Uhuru Kenyatta kwenda Ruto.
Ruto ambaye jana Mahakama ya Juu nchini humo ilibariki kuchaguliwa kwake baada ya kutupilia mbali pingamizi ya mshindani wake Raila Odinga ataapishwa Septemba 13, 2022 jijini Nairobi.
“Mgao wa Sh milioni 200 (Sh3.8 bilioni) chini ya Ofisi ya Rais umetolewa katika Hazina ya Kitaifa kwa ajili ya shughuli za Ofisi hiyo,” imeeleza Hazina ya Kenya katika ripoti ya Marekebisho ya Kiuchumi Kabla ya Uchaguzi iliyoripotiwa na chombo cha habri cha Daily Nation.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo kiasi hicho kimetengwa kwa kamati maalum inayohusika kusimamia na kuhakikisha Rais mpya anaingia madarakani baada ya siku sita zijazo.
Miongoni mwa shughuli zitakazofanyika kutoka na fedha hizo ni pamoja kuandaa sherehe ya aupisho, kukabidhi madaraka, ulinzi kwa Rais mteule, kuandaa vifaa na wafanyakazi muhimu kwa ajili ya Rais.
Sambamba na hayo inatarajiwa pia kuratibu taarifa za Rais mteule na maafisa husika wa umma na kurahisisha mawasiliano kati ya Rais anayemaliza muda wake na Rais mteule.
Zinazohusiana:
Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu umeigharimu Kenya zaidi ya Sh bilioni 856 zilizotengwa na hazina kukamilisha shughuli hiyo.
Kwa mujibu wa Katiba ya nchi hiyo, Rais Mteule ataapishwa siku saba baada ya Mahakama ya Juu kuidhinisha ushindi wa uchaguzi.
Baada ya kuapishwa, Rais atatia saini cheti cha kuapishwa na Rais anayemaliza muda wake atamkabidhi Rais vyombo vya mamlaka ikiwemo upanga na Katiba.
Bunge ndiyo litaweka utaratibu na sherehe za kuapishwa kwa Rais mteule. Jaji Mkuu ndiye atamwapisha Rais Mteule pamoja na msajili wa Mahakama ya Juu.