Watanzania 42 kutoka Israeli kurejeshwa leo
- Kundi la kwanza litarejea saa 6:55 katika Uwanja wa Ndege wa Abeid Amani Karume,Unguja na kundi la pili saa 11:55 jioni katika uwanja wa Julius Nyerere
Dar es salaam. Serikali ya Tanzania imetangaza kuwarejesha nyumbani Watanzania 42 kati ya 200 waliokuwa wamekwama nchini Israel kutokana na machafuko yanayoendelea kati ya taifa hilo na Iran kwa zaidi wiki mbili sasa.
Uamuzi wa kuwarejesha nyumbani raia hao ni utekelezaji wa mchakato wa Serikali wa kuwarejesha Watanzania wote waliokuwa wamekwama kwenye nchi hizo uliotangazwa June 20, 2025.
Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imesema Watanzania hao watawasili nchini leo Juni 25, 2025 kwa makundi mawili kupitia Ndege ya Shirika la Ethiopian Airlines.
Kundi la kwanza litawasili katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Abeid Amani Karume mjini Unguja saa 6:55 mchana, huku kundi la pili likitarajiwa kutua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam saa 11:55 jioni.
Kurejeshwa kwa raia hao kutoka Israel ni sehemu ya mpango wa Serikali wa kuwaondoa raia wake waliokwama katika maeneo yenye migogoro, kufuatia kuongezeka kwa hali ya hatari katika Mashariki ya Kati tangu Juni 13, 2025.
Katika kipindi hicho, kumeshuhudiwa mashambulizi ya anga na mashambulizi ya makombora baina ya Israel na Iran, kufuatia oparesheni ya kijeshi ya Israel “Operation Rising Lion” dhidi ya maeneo yanayotajwa kuwa ni vituo vya uzalishaji wa silaha za nyuklia nchini Iran.
Mashambulizi hayo yanakadiriwa kusababisha vifo vya watu zaidi ya watu 600 na majeruhi 5,332 tangu mashambulizi ya Israeli kuanza Juni 13, 2025 nchini Iran kama Wizara ya Afya chini humo ilivyoripoti na kati ya watu 24 mpaka 28 kwa upande wa Israel, ikiwemo vifo vya makamanda wa kijeshi na wataalamu wa nyuklia.
Wizara hiyo ilisema wiki iliyopita kuwa Watanzania waliopo Israel ni takriban 200, miongoni mwao wakiwa ni wafanyakazi wa ubalozi, wanafunzi pamoja na wataalamu mbalimbali ambao hadi kufiia Juni 20, 2025, 50 kati yao walijiandikisha kurejea nchini.
Serikali ya Tanzania imekuwa ikifanya uratibu kwa karibu kupitia Balozi zake zilizopo nchini Israel, Misri, Kuwait na Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), ambako Iran inawakilishwa kidiplomasia, kuhakikisha kila Mtanzania aliyeko katika maeneo hayo anafikiwa na kusaidiwa kurejea nyumbani salama.
Wakati watanzania 42 wakirejeshwa kutoka Israel bado kuna watanzania Watanzania 168 nchini Iran, ambao kwa mujibu wa wizara, wengi wao ni wanafunzi katika mji wa Qom (134) na wengine Tehran ambao Serikali imesema inaendelea kuratibu urejeshaji wa kundi hilo pia.
Aidha, Serikali imetoa wito kwa Watanzania walioko katika mataifa ya Mashariki ya Kati kuchukua tahadhari zote muhimu za kiusalama na kuwa tayari kwa maelekezo ya kuondoka, huku jumuiya ya kimataifa ikiendelea kutoa wito wa amani na utulivu katika eneo hilo lenye mivutano ya muda mrefu.
Latest
