ATCL kuwarudisha Watanzania waliokwama Dubai
- Safari hiyo itafanyika siku ya Jumapili Machi 8, 2026.
- Abiria wenye tiketi walioathirika na kusitishwa kwa safari za ndege Mashariki ya Kati kupewa kipaumbele.
Arusha. Shirika la Ndege la Tanzania (ATCL) limeandaa safari maalum kutoka Dar es Salaam kwenda Dubai kwa ajili ya kuwarudisha abiria waliositishiwa safari zao kufuatia vita vinavyoendelea kati ya Marekani, Israel na Iran.
Pia safari hiyo itawahusu abiria waliokwama nchini ambapo watasafirishwa hadi Dubai.
Taarifa ya ATCL iliyotolewa leo March 6, 2026 imeeleza kuwa safari hiyo itafanyika siku ya Jumapili Machi 8, 2026 maalum kwa abiria wenye tiketi walioathirika na kusitishwa kwa safari za ndege Mashariki ya Kati.
“Safari hii ya ndege imeandaliwa mahsusi kwa ajili ya kuwarejesha abiria majumbani mwao na sio safari ya kawaida ya kibiashara. Kipaumbele kitatolewa kwa abiria waliokuwa na tiketi halali za safari ya Dar es Salaam kwenda Dubai ambayo awali iliathirika,” imesema taarifa ya ATCL.

Moshi ukipanda angani baada ya shambulio la Israel katikaeneo la Beirut, kufuatia kuongezeka kwa mapigano kati ya Hezbollah na Israel wakati wa mzozo unaohusisha Marekani na Israel dhidi ya Iran nchini Lebanon. Picha | REUTERS/Mohamed Azakir.
Taarifa ya ATCL inakuja ikiwa zimepita siku tano tangu itangaze kusitisha safari zake kuelekea Dubai baada ya kufungwa kwa anga la Mashariki ya Kati kulikosababishwa na vita hiyo iliyoanza Februari 28, 2026.
Aidha, ATCL imewashauri abiria kuwasiliana na ofisi za shirika hilo kwa maelekezo na uthibitisho wa usafiri kabla ya kuondoka ikiwataka kutumia namba +255 748 773 900 kwa waliopo Dar es Salaam na namba +971 54 464 5322 kwa waliopo Dubai.
Awali Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ilisema inaendelea kufuatilia kwa karibu hali ya usalama inayoendelea Mashariki ya Kati huku ikiwataka wananchi waliopo eneo hilo kuchukua hatua stahiki kulinda usalama wao.
Mashambulizi ya Marekani na Israel yanalenga maeneo mbalimbali ya kijeshi ya Iran ikiwemo Mji Mkuu Tehran. Nchi hiyo nayo inajibu mapigo kwa kushambulia vituo vya kijeshi vya Marekani vilivyopo katika nchi jirani ikiwemo Dubai.
Mashambulizi hayo yamesababisha vifo vya watu zaidi ya 500 akiwemo Kiongozi Mkuu wa Iran, Ali Khamenei, aliyekuwa madarakani tangu mwaka 1989.
Latest