Wasafi TV yafungiwa miezi sita
- Ni baada yanakiuka Kanuni za Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta za mwaka 2018.
- Yadaiwa kutangaza maudhui yasiyofaa yaliyomuonyesha mwanamuziki Gigy Money akionesha utupu wake jukwaani.
- Yatakiwa pia kuomba radhi kwa umma wa Watanzania.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imekifungia kituo cha televisheni cha Wasafi TV kwa muda wa miezi sita kwa kutangaza maudhui yasiyofaa yaliyomuonyesha mwanamuziki Gigy Money akionesha utupu wake jukwaani.
TCRA imesema maudhui hayo yanakiuka Kanuni za Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta za mwaka 2018.
Kwa mujibu wa mamlaka hiyo, Mnamo Januari 1, 2021 majira ya 2:00 hadi saa 5:00 usiku kupitia kipindi cha “Tumewasha Live Concert” Wasafi Tv ilirusha maudhui jongefu yaliyokuwa yakimuonyesha msanii anayejulikana kwa jila la Gift Stanford Joshua Mwakyusa au “Gigy Money” akicheza katika jukwaa katika mitindo iliyokua ikionyesha utupu wa mwili wake.
UKIUKWAJI WA KANUNI ZA UTANGAZAJI ULIOFANYWA NA WASAFI TV 1.1.2021 pic.twitter.com/TRQOmVA2EB
— TCRA_TANZANIA (@TCRA_Tz) January 5, 2021
Kutokana na kosa hilo, TCRA imesitisha utoaji wa huduma ya matangazo za Wasafi TV kwa muda wa miezi sita kuanzia kesho Januari 6 hadi Julai 6, 2021.
Aidha, TCRA imeitaka runinga hiyo kuahirisha matangazo na kutumia muda uliobaki leo kuomba radhi kwa umma wa Watanzania kwa kukiuka kanuni za utangazaji.
“Iwapo Wasafi TV itashindwa, itakataa au itakaidi uamuzi huu, hatua zaidi za kisheria na kiudhibiti zitachukuliwa dhidi ya Wasafi TV,” inaeleza sehemu ya taarifa ya Kaimu Mtendaji Mkuu wa TCRA, Johanes Kalungule iliyotolewa leo Januari 5, 2021.
Zinazohusiana:
- LHRC yazungumzia adhabu ya vituo vitatu vya televisheni mtandaoni.
- TCRA yakusudia kusimamisha leseni za DSTV na Zuku.
- CCM yazidi kuongeza umiliki wa vyombo vya habari Tanzania
Wasafi TV iliyopata leseni ya kitaifa ya utoaji wa huduma ya maudhui ya kulipia kwa njia ya televisheni Agosti 2019 imekua kiungo muhimu kwa wasanii wa Tanzania kuonyesha kazi zao za muziki ambazo zimekuwa zikiwapatia kipato.
Hii itakuwa mara ya pili kwa chombo cha habari kinachomilikiwa na kampuni ya Wasafi Media kufungiwa kwa kukiuka kanuni za utangazaji. Septemba 11, 2020, TCRA iliifungia redio ya Wasafi FM kwa muda wa siku saba baada ya kutumia lugha za matusi kwenye vipindi vyake vya “The Switch” na “Mashamsham”.
Hata wakati, Wasafi TV ikifungiwa, Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) imemfungia Gigy Money kujihusisha na kazi za sanaa ndani na nje ya nchi kwa muda wa miezi sita, na kumuamuru kulipa faini Sh1 milioni.
BASATA imesema mwanamuziki huyo alivua gauni jukwaani na kubaki na vazi lililoonyesha maungo yake ya mwili wakati akitumbuiza jukwani jijini Dodoma Januari 1, 2021.
Latest
