Wasafi TV yapunguziwa adhabu, kurudi hewani Machi mosi
- Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetangaza kuipunguzia adhabu televisheni hiyo kutoka kifungo cha miezi sita na itarejea hewani Machi 1.
- Imepewa masharti matatu ikiwemo kutumikia adhabu yake mpaka tarehe tajwa.
- Uamuzi huo unatokana na Wasafi TV kukiri kosa na kuomba kupunguziwa adhabu.
Dar es Salaam. Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) imetangaza kuipunguzia adhabu televisheni ya Wasafi TV kutoka kifungo cha miezi sita na kuiruhusu kuendelea kurusha matangazo yake kuanzia Machi mosi mwaka huu, kwa masharti matatu ikiwemo kutumikia adhabu yake mpaka Februari 28.
Januari 5 mwaka huu, TCRA ilikifungia kituo hicho kwa muda wa miezi sita kwa kutangaza maudhui yasiyofaa yaliyokiuka Kanuni za Mawasiliano ya Kielektroniki na Posta za mwaka 2018.
Kwa mujibu wa mamlaka hiyo, mnamo Januari 1, 2021 majira ya 2:00 hadi saa 5:00 usiku kupitia kipindi cha “Tumewasha Live Concert” Wasafi Tv ilirusha maudhui jongefu yaliyokuwa yakimuonyesha msanii anayejulikana kwa jila la Gift Stanford Joshua Mwakyusa au “Gigy Money” akicheza katika jukwaa katika mitindo iliyokua ikionyesha utupu wa mwili wake.
Mkurugenzi Mkuu wa TCRA, James Kilaba amesema masharti hayo ni Wasafi TV kuendelea kutumia adhabu yake mpaka Februari 28 mwaka huu na baada ya hapo televisheni hiyo itaendelea kurusha matangazo yake.
“Wasafi TV inaelekezwa kuzingatia masharti ya leseni ya kutoa huduma ya maudhui kwa njia ya televisheni,” amesema Kilaba katika taarifa yake aliyoitoa leo Februari 4, 2020.
Sharti la tatu, Kilaba amesema iwapo Wasafi TV itashindwa, itakataa au kukaidi uamuzi huo, hatua zaidi za kisheria na kiudhibiti zitachukuliwa dhidi ya Wasafi TV.
Zinazohusiana:
- LHRC yazungumzia adhabu ya vituo vitatu vya televisheni mtandaoni.
- TCRA yakusudia kusimamisha leseni za DSTV na Zuku.
- Wasafi TV yafungiwa miezi sita
Uamuzi wa kuipunguzia adhabu televisheni hiyo, unatokana televisheni hiyo kuwasilisha maombi TCRA na vielelezo zaidi Januari 21 ikiomba kupitiwa upya kwa adhabu iliyotolewa ya miezi sita.
“Tarehe 28 Wasafi TV ilifika TCRA kwa ajili ya kusikilizwa maombi hayo,” amesema Kilaba na kubainisha kuwa televisheni hiyo iliwasilisha ushahidi mpya kuonyesha kuwa endapo ushahidi huo ungewasilishwa awali wakati wa usikilizwaji, TCRA ingeweza kutoa adhabu ya kufungiwa miezi sita.
Amesema pia Wasafi TV ilikiri kurusha matangazo mubashara kinyume na leseni yake na kuomba kupunguziwa adhabu yake.
Baada ya kusikiliza ushahidi wa televisheni hiyo, TCRA imetafakari uamuzi wake wa Januari 5 na sasa itairuhusu televisheni hiyo kuanza tena kurusha matangazo yake Machi mosi baada ya kukamilisha adhabu yake.
Latest
