Wanafunzi vyuo vikuu kuandaliwa mwongozo kukabiliana na ukatili wa kijinsia
- Ni wanaojiunga vyuo vikuu mkoani Mwanza.
- Serikali yasema utasaidia kuwapa elimu ya kujitambua na kukabiliana na matendo hayo.
Mwanza. Serikali mkoani Mwanza imesema itaandaa muongozo utakaowasaidia wanafunzi wanaojiunga na vyuo vikuu mkoani humo kufahamu kwa kina mbinu za kujikinga na ukatili wa kijinsia wanapoendelea na masomo yao.
Katibu Tawala Mkoa wa Mwanza, Ngussa Samike amesema wanatambua kuwa vijana wanaoingia vyuoni kwa mwaka wa kwanza hufanyiwa ukatili wa kingono na dada zao au kaka zao.
Amesema pamoja na hao pia kuna jamii inawaangalia na wanakumbana na vishawishi vingi ambavyo huwarubuni na kuwapotezea mwelekeo wa maisha.
“Kama mkoa tutakaa tuangalie namna gani tuandae mwongozo kwenye vyuo vyetu ili uwasaidie vijana hao waweze kujitambua,” amesema Samike jana Juni 8, 2022 katika mdahalo ulioandaliwa na Shirika la Wadada Solution kuhusu umuhimu wa afya ya uzazi na kupinga ukatili kwa ustawi wa vijana na maendeleo ya Taifa.
Katibu tawala huyo ametumia fursa hiyo kuwatahadharisha vijana kujitambua na kutofanya maamuzi ambayo yanaweza kuleta athari kwenye jamii na kuharibu kesho yao.
“Ni vyema kulinda afya kwa kuwa hiyo ni ya kwako lakini ikiharibika itaharibu maisha yako kiujumla lakini pia itaharibu maisha ya ndugu na jamii inayokuzunguka hivyo ni wajibu wa kila mmoja kuhakikisha analinda afya yake kwa manufaa ya siku zijazo,” amesema Samike.
Akizungumzia suala la ukatili wa kijinsia shuleni, Samike amesema vitendo hivyo vimekithiri na kwamba baadhi ya wanafunzi hawapati alama wanazositahili katika masomo yao kwa sababu wanashawishika kuingia katika rushwa ya ngono.
Amesema ukatili unaathiri zaidi kisaikolojia kulingana na vitendo ambavyo mtu au mtoto anatendewa kutoka kwa ndugu au mtu yeyote ambaye anamfanyia ukatili.
Soma zaidi:
- Jinsi ya kufanya mitandao ya kijamii isikuharibie mahusiano yako
- Yaliyojificha nyuma ya mahusiano, ndoa zinazoanzia mtandaoni
- Unyanyasaji wachangia kuwakimbiza wasichana kwenye mitandao ya kijamii
Bila kutaja takwimu, Katibu tawala huyo amesema zipo kesi kadhaa za ukatili wa kijinsia kwa watoto wadogo ambazo kama mkoa wanazifuatilia.
“Niwaombe sana mnapofanyiwa ukatili msipuuzie kutoa taarifa, na hii imekuwa kawaida wanapofanyiwa ukatili wanakaa kimya hata kama majirani wameshuhudia nao wananyamaza, ni tofauti na nchi za wenzetu ambapo mtu anapofanyiwa ukatili anachukua hatua haraka kwenda kuripoti,” amesema.
Awali Mkurugenzi wa Shirika la Wadada Solution, Lucy John amesema katika kukabiliana na vitendo vya ukatili wanatoa elimu kuhusu afya ya uzazi na stadi za maisha kwa wanafunzi wa ngazi mbalimbali zikiwemo za msingi hadi vyuo.
Amesema kwenye kipengele cha elimu ya ukatili wa kijinsia, shirika linatoa elimu kwa wanafunzi kubaini viashiria vinavyoashiria vitendo hivyo huku kwa wnafunzi wa sekondari wanawaelimisha pia masuala ya uongozi na afya ya uzazi.
“Kama shirika tunawasaidia vijana wakiona viashiria hivi ni dalili ya ukatili lakini kwa upande wa vyuo tunatoa elimu waweze kujua kijikinga na vitendo hivyo,” amesema John.
Makamu Mkuu wa Chuo cha Saut-Taaluma Profesa Hosea Rwegoshora, amewasihi vijana kuzingatia elimu inayofundishwa shuleni ili iwasaidie katika vizazi vijavyo.
“Shida kubwa iliyopo kwa sasa ni vijana kuzaliwa kipindi ambapo utandawazi umezidi hivyo kijana hapati elimu ya afya ya akili na uzazi kwa kiwango kile ambacho watu wa zamani walikuwa wanapata, siku hizi utandawazi umekuwa ndio elimu yao kuu na vijana wengi hawazingatii tena maadili na maelekezo ya wazazi wao,” amesema Prof Rwegoshora.
Latest
