Walioondolewa kazini kwa kughushi vyeti kulipwa michango yao kuanzia Novemba

October 26, 2022 10:53 am · Mwandishi
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni baada ya Rais Samia kuridhia.
  • Walioondolewa katika utumishi wa umma Oktoba 2016 hadi Aprili mwaka 2017.
  • Wataanza kulipwa Novemba mosi mwaka huu.

Dar es Salaam. Watumishi wa umma walioondolewa kazini kwa kughushi vyeti wataanza kurejeshewa michango yao waliyochangia kwenye Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kuanzia Novemba Mosi mwaka huu. 

Watumishi hao ni wale walioondolewa katika utumishi wa umma wakati wa zoezi la uhakiki wa vyeti lililoendeshwa katika kipindi cha kuanzia Oktoba 2016 hadi Aprili mwaka 2017.

Uhakiki huo uliowatoa katika mfumo wa utumishi wa umma watumishi wasiopungua 14,516 waliobainika kuwa na vyeti vya kughushi.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu, Profesa Joyce Ndalichako akizungumzia kuhusu uamuzi huo leo Oktoba 26, 2022 amesema Rais Samia Suluhu Hassan ameridhia watumishi hao warejeshewe michango yao waliyochangia wakati wakiwa kwenye utumishi. 

“Kufuatilia maelekezo hayo, mifuko ya Hifadhi ya Jamii PSSSF na NSSF itarejesha michango ya wafanyakazi iliyowasilishwa kwenye mifuko hiyo bila kuhusisha michango ya mwajiri,” amesema Prof Ndalichako. 

Zoezi la kuwarejeshea michango hiyo litaanza kufanyika kuanzia Novemba Mosi mwaka 2022 kwa njia ya benki na siyo pesa taslimu.

Prof Ndalichako amesema mtumishi husika aliyeondolewa kazini atapaswa kwenda kwa aliyekuwa mwajiri wake akiwa na picha mbili za ‘passport size’, nakala ya taarifa za benki (Bank Statement) ya akaunti iliyo hai na nakala ya kitambulisho cha Taifa au mpiga kura au leseni ya udereva.

Pia mtumishi atatakiwa kujaza hati ya ridhaa kwa aliyekuwa mwajiri wake.

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW