Uzushi: Magufuli hajasheherekea kwa kucheza ngoma kumalizika kwa Corona
- Baadhi ya watu wamezusha kuwa Corona imetokomezwa Tanzania na Rais Magufuli amesheherekea kwa kucheza ngoma.
- Habari hiyo ambayo iko kwenye mfumo wa video ni uzushi haina ukweli wowote.
Dar es Salaam. Kama umesikia habari inayomuelezea Rais John Magufuli akisheherekea kumalizika kwa ugonjwa wa Corona nchini Tanzania kwa kucheza ngoma, basi fahamu kuwa huo ni uzushi mtupu.
Habari hiyo iliwekwa kwenye mtandao wa Facebook kwa mara ya kwanza Mei 2020 ikiwa na maelezo ya kiingereza “No masks. No social distancing. No curfews. No lockdown – Tanzania celebrations after defeating corona”
Ikiwa na maana kuwa “Hakuna barakoa, Hakuna umbali wa mita moja, hakuna kujifungia ndani- Watanzania wanashangilia baada ya kuishinda corona,”
Baadaye habari hiyo ilisambazwa katika mitandao mbalimbali zikiwemo akaunti za Facebook za Uganda.
Zinazohusiana:
- Picha za tetemeko Croatia zilivyotumika kupotosha Corona mtandaoni
- Siyo kweli wananchi Italia wanatupa pesa mitaani kuepuka Corona
Ukweli wa habari hiyo ikoje
Timu ya Nukta Fakti imebaini kuwa habari hiyo iliyopo kwenye mfumo wa video siyo ya kweli kwa sababu hakuna mahali ambapo Rais Magufuli na Watanzania walishiriki sherehe ya ngoma kwa ajili ya ushindi dhidi ya Corona.
Video hiyo ni ya mwaka 2016 wakati wa sherehe ya uzinduzi wa hosteli za Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam (UDSM) na haiusiani na janga la Corona.
Rais Magufuli katika hotuba zake za hivi karibuni ikiwemo aliyotoa Juni 16,2020 wakati anavunja Bunge la 11 aliagiza la kufunguliwa kwa shule zote Juni 29, 2020 sambamba na shughuli nyingine zote baada ya Corona kupungua kwa kiasi kikubwa nchini.
Hata hivyo, katika hotuba hizo, Rais amekuwa akirudia mara kadhaa kuwa Watanzania wanapaswa kuendelea kuchukua tahadhari ya kujikinga na ugonjwa huo kwa kufuata miongozo ya wataalam wa afya.