Usomaji vitabu bado bado Tanzania
- Wasomi wasema watu wanakosa maarifa kwa sababu hawasomi.
- Waanza kutoa hamasa kuongeza idadi ya wasomi.
- Serikali yakarabati maktaba kuvutia watu kusoma vitabu.
Mwanza. Elimu ikiwa ni msingi mkuu wa maendeleo kwa taifa lolote ulimwenguni, Watanzania wameaswa kujenga utamaduni wa kusoma vitabu kupata maarifa yaliyohifadhiwa kwa njia ya maandishi.
Balozi Ombeni Sefue ametoa rai hiyo akiwa mgeni rasmi kwenye Kongamano la Kigoda cha Uprofesa cha Hayati Rais Benjamin Mkapa lililofanyika katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustine Tanzania (SAUT) kampasi ya Mwanza, Jumamosi Novemba 12, 2022.
“Hayati Mkapa alipenda kusoma vitabu na majarida kuliko kutumia muda wake mwingi kupiga domo kuhusu mambo yasiyo na msingi au vikao vya kupewa sifa,” amesema Balozi Sefue.
Balozi Sefue amebainisha kuwa utaratibu wa kusoma vitabu humfanya msomaji kuwa na uwezo mkubwa wa kujenga hoja na kupata mawazo mapya ambayo hayakuwepo hapo awali.
Akimtolea mfano Hayati Mkapa aliyesifika kwa kujenga hoja imara kwenye makongamano na mijadala mbalimbali, Balozi Sefuye amesema kuwa hayo ni miongoni mwa matunda ya utamaduni wa kusoma vitabu.
Uimara wa falsafa za Hayati Mkapa ukijengwa na utaratibu wa usomaji wa vitabu mbalimbali, Mwanafalsafa na mhadhiri wa SAUT Innocent Sanga amesema kuwa kiongozi huyo alikuwa na msimamo katika hoja zake.
Mkuu wa Mkoa wa Mwanza Adam Malima amefafanua kuwa Hayati Mkapa alisifika kwa mawazo chanya kufuatia ufatiliaji wake wa mambo muhimu yaliyojificha katika maandishi.
Utamaduni wa kusoma vitabu umetajwa kuwa changamoto kwa kizazi cha sasa ambapo kundi kubwa hawana kuhusu suala hilo.
Washiriki wa Kongamano la Kigoda cha Uprofesa cha Hayati Rais Benjamin Mkapa lililofanyika mkoani Mwanza Oktoba 12, 2022. Picha | Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mwanza.
Hali ya usomaji wa Vitabu
Leah Ibrahim Mkazi wa wilaya ya Nyamagana jijini Mwanza katika mahojiano na Nukta Habari (www.nukta.co.tz) amesema kuwa hupendelea kusoma vitabu vya dini kama Biblia akiamini kuna mafundisho mengi ila hufanya hivyo wakati wa ibada pekee.
Mkazi mwingine Victor Godfrey Lusega amesema tangu amalize elimu ya sekondari hakumbuki mara ya mwisho kusoma kitabu chochote kwani muda wake mwingi anatumia kutafuta riziki.
Hili ni tofauti kwa Oppa Ezekiel Choga ambaye hupenda kusoma vitabu mara kwa mara kutokana na hamu yake ya kujifunza misamiati mipya na kupata mawazo chanya kufikia maendeleo.
Soma zaidi:
- Anna Nkyalu: Ukosefu wa ajira ulivyomfungulia fursa ya kufaidika na kipaji cha uchoraji
- Kutana na mwanamke mjasiriamali anayeboresha maisha watoto, wanawake Tanzania
- Jessica Mshama: Mwanamuziki, Mjasiriamali anayebadilisha maisha ya Watanzania kwa biashara
Sababu za watu kutopenda kusoma vitabu
Mwanasaikolojia na Mhadhiri SAUT Leons Maziku amesema baadhi ya watu hupenda njia ya mkato kufikia mafanikio na hatimaye hukosa hamasa ya kutafuta vitu muhimu vilivyohifadhiwa kwenye maandishi.
“Tatizo watu wengi wanapenda short cut way (njia ya mkato) ili kufanikiwa, kila kitu kina njia yake ya mafanikio na nidhamu ya mafanikio lazima uwe nayo,” amesema Maziku.Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Elimu Tanzania (TET) Dk Aneth Komba katika tamasha la 13 la kimataifa la vitabu Tanzania lilofanyika Oktoba 11 hadi 15 mwaka huu, alisema kuwa hamasa bado ni ndogo kwa jamii kushiriki usomaji wa vitabu mbalimbali.
“Tunashirikina na kuhamasisha ari mpya ya usomaji na tutaendelea kuhimiza ari ya usomaji wa vitabu, tusome vitabu vyote kwa ajili ya kupata maarifa,’’ alisema Dk Komba.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Waziri Profesa Adolf Mkenda wakati akiwasilisha bajeti ya wizara yake kwa mwaka 2022/23, alisema kuwa Serikali imeanza kujenga utamaduni wa kusoma vitabu kwa kuanza na wanafunzi.
Prof Mkenda alieeleza kuwa wizara imeanza kwa kugawa vitabu shuleni ili kuwajengea utamaduni wanafunzi kujisomea wakiamini ndiyo taifa la kesho.
Wizara yake ilitoa ushauri wa kitaaluma katika vituo 286 kati ya 350 vya huduma ya maktaba na kuboresha maktaba za mkoa ikilenga kuongeza idadi ya wanaosoma vitabu nchini.
Prof. Mkenda alisema kuwa takriban Sh1 bilioni zimetengwa kufadhili uzalishaji wa vitabu kwa mwaka wa fedha 2022/23 ili kuhamasisha Watanzania kusoma kwa wingi vitabu.
Latest
