Thamani ya sarafu za nje yaimarika dhidi ya Shilingi

August 14, 2024 8:11 pm · John Francis
Share
Tweet
Copy Link
  • Ni sarafu za Dola, Euro, Paundi, Yuan na Randi.
  • Yuan yaongoza kwa ongezeko la asilimia 3.27.

Dar es Salaam. Viwango vya kubadili baadhi ya fedha za kigeni dhidi ya Shilingi ya Tanzania vimeongezeka kidogo ndani ya mwezi mmoja, karibia asilimia moja, kuanzia Julai 15 hadi Agosti 14, mwaka huu.

Fedha hizo za kigeni zilizoonekana kuimarika dhidi ya Shilingi ya Tanzania ni pamoja na Euro ya Ulaya , Paundi ya Uingereza, Dola ya Marekani, Yuan ya China, pamoja na Randi ya Afrika kusini.

Viwango vya kubadili fedha za kigeni vilivyotolewa leo Agosti 14, 2024 na Benki kuu ya Tanzania (BoT) vinaonesha kuwa kwa wastani thamani ya Paundi dhidi ya Shilingi ya Tanzania imepanda kutoka Sh3,407 hadi Sh3,431 ndani ya mwezi mmoja, sawa na ongezeko la asilimia 0.69. 

Dola ya Marekani nayo imepanda kwa wastani kutoka Sh2,627 hadi Sh2,679 ndani ya mwezi mmoja, sawa na ongezeko la asilimia 1.98. 

Ongezeko hili linaweza kuathiri biashara za Tanzania zinazotegemea malipo kwa Dola ya Marekani

Thamani ya Euro dhidi ya Shilingi ya Tanzania nayo imepanda kwa wastani kutoka Sh2,861 hadi Sh2,931 ndani ya mwezi mmoja, ikiwa ni ongezeko la asilimia 2.43. 

Kwa Yuan ya China, ongezeko ni sawa na asilimia 3.27, thamani ya Yuan imepanda kwa wastani kutoka Sh362 hadi Sh374 ndani ya mwezi mmoja.

Ongezeko hili linaweza kuongeza gharama za bidhaa kutoka China hususan wafanyabiashara wanaonunua bidhaa za jumla kutoka China na kuja kuziuza nchini.

Wafanyabiashara hawa watalazimika kulipa zaidi kwa bidhaa na huduma zinazotoka nje, hivyo kupunguza faida zao au kuwalazimisha kuongeza bei kwa wateja wa ndani.

Hata hivyo, mfumuko wa bei umeendelea kusalia ndani ya wigo wa Serikali wa chini ya asilimia tano ambapo kwa mwaka ulioishia Julai 2024, Tanzania ilirekodi kiwango cha mfumuko wa bei wa asilimia 3 ambacho kilishuka kutoka asilimia 3.1 iliyorekodiwa mwezi Juni.

Randi ya Afrika Kusini nayo imepanda kwa wastani kutoka Sh146 hadi Sh148 ndani ya mwezi mmoja, sawa na ongezeko la asilimia 1.14.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...

Enable Notifications OK No thanks