Thamani miamala ya kifedha kwa njia ya simu yapungua, watumiaji wakiongezeka

October 27, 2022 1:36 pm · Daniel Samson
Share
Tweet
Copy Link
  • Yapungua kwa Sh19.09 bilioni ndani ya mwezi mmoja.
  • Watumiaji na idadi ya miamala waliyofanya yaongezeka. 

Dar es Salaam. Ripoti mpya ya Takwimu za Mawasiliano ya Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA) inaonyesha kuwa miamala inayofanywa kupitia huduma za kifedha za simu za mkononi imepungua kwa Sh19.09 bilioni ndani ya mwezi mmoja.

Ripoti hiyo ya robo ya tatu ya mwaka 2022, inabainisha kuwa mwezi Septemba pekee thamani ya miamala ya fedha iliyofanywa katika simu za mkononi ilikuwa Sh12.72 trilioni kutoka Sh12.74 trilioni iliyorekodiwa Agosti mwaka huu.

Huduma za kifedha za kwenye simu zinasaidia kuongeza mzunguko wa fedha nchini na kutatua changamoto mbalimbali za kibenki ikiwemo kuweka fedha, kukopa na kulipia huduma na bidhaa mbalimbali.

Licha ya thamani ya miamala hiyo kupungua, miamala kwa njia ya simu iliyofanywa Septemba imeongezeka hadi milioni 366.17 kutoka miamala milioni 356.79 ya mwezi uliotangulia. 

Kwa wastani Septemba mtu mmoja alikuwa anafanya miamala ya kifedha tisa kwenye simu yake yenye thamani ya 321,341. 

TCRA katika ripoti hiyo, imeeleza kuwa idadi ya watumiaji wa huduma za kifedha kwa njia ya simu imeongezeka hadi watu milioni 39.5 Septemba mwaka huu kutoka watumiaji milioni 38.5 wa mwezi Agosti.

Kampuni ya Vodacom inayomiliki M-Pesa ndiyo inamiliki sehemu kubwa ya soko la huduma za kifedha kwa njia ya simu kwa asilimia 39 ikifuatiwa na Tigo (asilimia 25) na Airtel kwa asilimia 23. 

Follow Us on TikTok

FOLLOW NOW

Subscribe to Our YouTube Channel

SUBSCRIBE NOW