Teknolojia inavyoweza kuboresha miundombinu, mawasiliano nchi za SADC
- Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema zinapaswa kuwekeza katika uunganishaji na uwianishaji wa viwango mbalimbali vya Tehama.
- Amesema kuna haja ya kuboresha miundombinu muhimu ya usafirishaji, utaratibu wa ugavi na usafirishaji wa vitu na huduma.
Dar es Salaam. Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amesema ili kuleta maendeleo endelevu ya viwanda, kuongeza biashara na kutengeneza ajira, nchi wanachama wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) zinapaswa kuwekeza katika uunganishaji na uwianishaji wa viwango mbalimbali vya Tehama.
Amesema hatua hiyo itasaidia kutatua changamoto za maendeleo ya miundombinu na muingiliano wa mawasiliano nje ya mipaka ya nchi na kikanda.
“Changamoto hizo zinajumuisha maunganisho ya njia kuu za mawasiliano kati ya nchi jirani, kuyafanya mawasiliano ya kikanda yabaki ndani ya kanda, maunganisho ya kuvuka mipaka ya nchi, upangaji wa bei pamoja na uwianishaji wa viwango,” amesema Majaliwa.
Majaliwa alikuwa akizungumza jana (Septemba 19, 2019) wakati akifungua mkutano wa pamoja wa mawaziri wa SADC wa sekta ya Tehama, uchukuzi na hali ya hewa jijini Dar es Salaam.
Zinazohusiana:
- Mambo muhimu yatakayozisaidia kampuni zinazochipukia Tanzania kukua
- Startups za Tanzania zilizotamba mwaka 2018
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Waziri Mkuu, nchi wanachama zinapaswa kuhakikisha kuwa utekelezaji unalenga katika teknolojia zinazochipukia kwenye utoaji wa huduma za posta sambamba na kuanzisha huduma na bidhaa mpya ambazo zitakidhi mahitaji ya sasa ya wateja na kuhamasisha biashara ya mtandao.
“Katika kufanikisha hili, ni muhimu kufanya tathmini ya utekelezaji wa Mkakati wa Posta wa SADC wa mwaka 2017-2020 ambao uliridhiwa mwezi Septemba, 2017,” amesisitiza Majaliwa.
Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu amesema ili kufikia mtangamano wa kikanda kuhusu miundombinu ya usafiri na usafirishaji, mkutano huo unapaswa kuzungumza namna gani nchi wanachama zinaweza kuwianisha sera, viwango, mifumo ya sheria katika maeneo ya barabara, reli, usafiri wa anga, usafiri wa majini, pamoja na hali ya hewa.
Waziri Mkuu amesema kuna haja ya kuboresha miundombinu muhimu ya usafirishaji, utaratibu wa ugavi na usafirishaji wa vitu na huduma pamoja na kuwezesha kutoa mizigo kutoka sehemu moja kwenda sehemu nyingine ndani ya kanda.
“Hivyo, nawaomba katika mkutano wenu mjadili maeneo haya na kuja na mapendekezo ya suluhisho ili kutatua vikwazo mbalimbali,” amesema Majaliwa.