TCU yafungua udahili awamu ya pili mwaka wa masomo 2025/26
Arusha. Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) imefungua dirisha la udahili kwa awamu ya pili kwa wanafunzi wa shahada ya kwanza mwaka wa masomo 2025/2026 kuanzia leo Jumatano, Septemba 3 hadi 21, 2025.
Dirisha hilo linafunguliwa wakati ambao waombaji 146,879 sawa na asilimia 79.4 ya waombaji walioomba udahili katika awamu ya kwanza wamepata udahili kwenye vyuo walivyoomba ikitarajiwa kuongezeka zaidi kupitia udahili wa awamu ya pili na nyinginezo
Taarifa ya Katibu Mtendaji wa TCU, Dk Charles Kihampa imebainisha kuwa kufunguliwa kwa dirisha hilo ni fursa kwa waombaji ambao hawakuweza kutuma maombi ya udahili au hawakuweza kupata nafasi ya kudahiliwa katika awamu ya kwanza kutokana na sababu mbalimbali.
“Tume inawaasa waombaji ambao hawakuweza kutuma maombi ya udahili au hawakuweza kupata nafasi ya kudahiliwa katika Awamu ya Kwanza kutokana na sababu mbalimbali, watumie fursa hii vizuri kwa kutuma maombi yao ya udahili kwenye vyuo wanavyovipenda…
….Tume inaelekeza Vyuo vya Elimu ya Juu nchini kutangaza programu ambazo bado zina nafasi. Waombaji udahili na vyuo wanapaswa kuzingatia utaratibu wa udahili wa Awamu ya Pili kama ilivyooneshwa kwenye kalenda ya udahili iliyoko katika tovuti ya TCU,” imesema taarifa ya Kihampa.
TCU imewataka waliodahiliwa katika chuo zaidi ya kimoja kuthibitisha udahili wao katika chuo kimojawapo kuanzia leo hadi 21 Septemba, 2025.
Uthibitisho huo unafanyika kwa kutumia namba maalum ya siri iliyotumwa kwa ujumbe mfupi kupitia namba zao za simu au barua pepe zilizotumika wakati wa kuomba udahili huku wasiopata kwa wakati ujumbe huo, wakishauriwa kuingia kwenye mifumo ya udahili ya vyuo walivyodahiliwa na kuomba kutumia namba hizo za siri.
Aidha, uthibitisho wa udahili ufanyike kupitia akaunti ambayo muombaji alitumia wakati wa kuomba udahili. Kwa urahisi wa rejea, orodha ya majina ya waliodahiliwa katika chuo zaidi ya kimoja inapatikana kwenye tovuti ya TCU (www.fou.go.tz).
Latest