“Startups” za Tanzania zapewa somo la uwazi, uwajibikaji kuvutia mitaji ya uwekezaji

August 24, 2019 8:02 am · Rodgers Raphael
Share
Tweet
Copy Link
  • Zimekumbushwa kujenga mifumo imara ya usimamizi wa biashara zinazoweza kutengeneza faida endelevu.
  • Zatakiwa kujiendesha kwa uwazi na kuwajibika kwa matumizi mazuri ya fedha. 
  • Elimu na mafunzo ya uwekezaji kuzibeba zaidi. 

Dar es Salaam. Kampuni changa (Startups) za Tanzania zimeshauriwa kujenga mifumo imara ya usimamizi  wa biashara ili kujiweka katika nafasi ya kuvutia wawekezaji wanaoweza kuwekeza mitaji yao itayozisaidia kukua na kupata faida. 

Kampuni hizo ni zile zilizojikita katika ujasiriamali wa kutumia teknolojia kutatua changamoto za jamii.

Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya SSC Capital inayojishughulisha na usimamizi wa biashara na ukuzaji wa mitaji, Salum Awadh aliyekuwa akizungumza jana (Agosti 23, 2019) na wamiliki wa kampuni jijini Dar es Salaam, amesema kampuni nyingi changa za Tanznaia hazijui namna ya kuandaa mawazo ya biashara ili kufikia kiwango cha kuvutia wawekezaji.

“Watanzania hawana mifumo mizuri ya biashara inayovutia wawekezaji,” Amesema Awadh.

Amesema ziko kampuni nyingi ambazo zinahitaji kuwekeza mitaji yao, lakini zinasita kwa sababu zinaogopa kuwekeza mitaji kwenye biashara ambazo hazina muundo na mipango iliyo wazi ambayo inaweza kuzalisha faida endelevu. 

Kwa mujibu wa Awadh, kampuni za Kenya, Nigeria na Afrika Kusini zimekuwa zikifanya vizuri kuvutia mitaji ya uwekezaji kuliko Tanzania kwa sababu zina uelewa mpana wa uwekezaji na jinsi ya kujiendesha katika mfumo unaotambulika kimataifa.

Amebainisha kuwa bado kampuni hizo zina nafasi ya kujiimarisha na kuweka mambo sawa ili kuongeza kasi ya kuwafikia watu wengi katika jamii, endapo zitaamua kubadilika ili kuaminiwa na wawekezaji. 


Soma zaidi:


Mtaalam wa Masoko, Elizabeth Riwa ambaye alishiriki mafunzo hayo amesema makampuni na hata wafanyabiashara wanahitaji kujiendeleza kielimu kwa kujiunga na vituo atamizi “Hubs” mbalimbali ambazo zinawasaidia katika kuendeleza mawazo yao ili kuimarisha biashara zao ili kuvutia wateja na wawekezaji.

“Kama mfanyabiashara, haijalishi ngazi ya elimu uliyonayo cha msingi ni kuwa tayari kujifunza kwa kuhudhuria semina zinazotoa mafundisho yanayolenga kukuza biashara. Semina nyingi ni bure na zina manufaa kwa ukuaji wa biashara,” amesema Riwa.

Pia amewataka wamiliki wa startups kujenga mifumo ya wazi na uwajibikaji ya matumizi ya fedha katika kampuni zao ili kuondoa mashaka wakati wakisaka mitaji.

“Makampuni mengi huonyesha kitu wanachokifanya na suluhisho wanalotoa lakini wanashindwa kueleza kwa uwazi ni namna gani muwekezaji anapata pesa yake,” amesema Riwa.

Follow Us on TikTok

Subscribe to Our YouTube Channel

Subscribe

Loading videos...

Loading videos...

Loading videos...