Fursa nyingine ya mitaji, mafunzo kwa ‘startups’ za Tanzania
- Ni zile zinazostahimili athari za Corona na zenye kutoa suluhu za kiuchumi na kijamii.
- Kampuni zinazochipukia ama ‘startups’ 10 zitakazofanya vizuri zitapata mitaji na mafunzo kuendeleza kazi zao.
- Shindano hilo linalenga kuongeza fursa za ajira kwa vijana na wanawake wajasiriamali Tanzania.
Dar es Salaam. Kampuni zinazochipukia Tanzania (startups) zimefunguliwa fursa ya kuingia katika shindano maalum la kutafuta suluhu zitakazosaidia shughuli za kiuchumi na jamii kurejea na kustahimili wakati huu ambao dunia inakabiliwa na janga la ugonjwa wa virusi vya Corona.
Shindano hilo lililopewa jina la “Recovery and Resilience Innovation Challenge” limeandaliwa na Programu ya Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (UNDP), Ubalozi wa Uholanzi nchini Tanzania na Mfuko wa Ubunifu na Maendeleo ya Watu (HDIF).
Taarifa ya pamoja iliyotolewa na kampuni ya Seedstars Dar es Salaam na kituo atamizi cha Ndotohub watakaotekeleza programu ya shindano hilo inaeleza kuwa watatoa mafunzo na tuzo kwa kampuni zitazokazoshinda zenye huduma na bidhaa zinazostahimili mtikisiko wa soko katika kipindi hiki cha janga la COVID-19.
“Kipaumbele katika shindano hili kitatolewa kwa biashara zinazomilikiwa na vijana na wanawake. Biashara zitakazoshiriki zinatakiwa ziwe zinatumia teknolojia kutoa suluhu ya pengo lilionekana wakati wa COVID-19,” amesema Mkurugenzi Mkaazi wa HDIF, Joseph Manirakiza katika taarifa hiyo.
Bosi huyo wa HDIF amesema moja ya sifa ya kampuni kushiriki shindano hilo ni uwepo wa mawazo yaliyo tayari kuyafanyiwa kazi nchini Tanzania katika sekta za utalii, kilimobiashara, afya, elimu na maji, usafi na kujisafi (WASH).
Soma zaidi:
- Mambo muhimu yatakayozisaidia kampuni zinazochipukia Tanzania kukua
- Startups za Tanzania zilizotamba mwaka 2018
- Starups nne Zanzibar zapenya shindano la Seedstars
Katika shindano hilo, startups 20 zitachaguliwa kuingia katika programu maalum ambapo 10 kati ya hizo zitapata mitaji na mafunzo maalum ya miezi mitatu ya kuendeleza kazi zao.
“Uholanzi tunaamini kuwa kuna umuhimu wa kuzisaidia na kuzitambua biashara ndogo zenye ubunifu na suluhu dhidi ya athari za COVID-19,” amesema Lianne Houben, Naibu Balozi wa Ubalozi wa Uholanzi nchini Tanzania.
Balozi huyo amesema wanataka kuzitambua startups hizo ambazo zimehimili mbadiliko yaliyoletwa na COVID-19 ili ziwe kielelezo kwa kampuni zingine kukua hata kipindi chenye changamoto nyingi.
UNDP, mdau wa programu inaamini kuwa kuwawezesha vijana wa Tanzania kuwa wavumbuzi na wafanikiwe katika ujasiriamali itasaidia kufikia malengo ya Malengo ya Mendeleo Endelevu (SDG’s) na kutengeneza fursa za ajira.
Latest