Sababu mwandishi wa TBC kufariki akishuka Mlima Kilimanjaro
- Kifo hicho kimetokana na ajali ya baiskeli aliyokuwa akiendesha wakati akishuka mlima huo.
- Alifariki wakati ametoka katika uzinduzi wa intaneti kwenye kilele cha mlima huo.
Dar es Salaam. Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania (TANAPA) limesema kifo cha aliyekuwa mwandishi wa habari wa Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) Joachim Kapembe kimesababishwa na ajali ya baiskeli iliyotokea ndani ya hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro.
Kifo cha Kipembe (45) kimetokea Disemba13, 2022 majira ya saa 12:00 jioni katika kituo cha Kibo (Kibo Hut) kuelekea kituo cha Horombo.
“Mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa ya Kanda ya Kaskazini (KCMC) iliyopo Moshi.,” imesema taarifa ya Tanapa iliyotolewa na leo Disemba 14, 2022 na kusainiwa na Afisa Mwandamizi wake Catherine Mbena.
Kapembe ambaye enzi za uhai wake alikuwa mtumishi wa TBC alikuwa mmoja kati ya watu waliopanda Mlima Kilimanjaro Disemba 13, 2022 wakati wa kwenda kuzindua mtandao wa intaneti katika kilele cha Uhuru.
Soma zaidi
-
Mke adaiwa kumuua mume wake akishirikiana na watoto
-
Mambo ya kujifunza baada ya mgao wa maji kupungua Dar
Huduma hiyo ya intaneti ilizinduliwa na Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Nape Nnauye ambapo inatajwa itarahisisha upatikanaji wa mawasiliano ya kimtandao kwenye mlima huo, mrefu kuliko yote Afrika.
Hatua hiyo inaelezwa kuwa inaweza kuongeza idadi ya watalii wanaotembelea mlima huo kwa shughuli za utalii na hivyo kuongeza mapato kwa Serikali na ajira kwa watu wakiwemo waongoza watalii.
“Tunataka tuangaze sana, tuconnect (tuunganishe) kilele kikubwa sana cha bara letu na wote watakaokuja kutembelea…nataka tukio hili litumike kuwafanya Watanzania wajivunie nchi yao,” alisema Nape kwenye hafla iliyoandaliwa kabla ya kupanda mlima huo.
Waziri Nape aliongozana na viongozi mbalimbali kwenye uzinduzi huo akiwemo Msemaji Mkuu wa Serikali Gerson Msigwa, wanahabari, timu ya madtari, wapagazi na watalii wengine kutoka ndani na nje ya nchi.
Latest