Ijumaa, Mei 03, 2024
Dar es Salaam. Miaka sita ijayo yaani mwaka 2025, Serikali imeadhimia kuwa Tanzania itakuwa ni nchi yenye uchumi wa kati unaoendeshwa na sekta ya viwanda. Lakini, uliwahi kujiuliza ni mikoa gani inaongoza kwa wafanyakazi wengi wanaojishughulisha viwandani?
Mwishoni mwa mwaka jana Ofisi ya Taifa ya Takwimu (NBS) ilichapisha Ripoti ya Utafiti wa Uzalishaji Viwandani ya mwaka 2016 (Annual Survey of Industrial Production 2016) inayobainisha kuwa mwaka huo kulikuwa na watu 221,688 waliokuwa wakijihusisha viwandani.
Hata hivyo, ripoti hiyo iliyofanywa na NBS kwa ushirika na Wizara ya Viwanda, Biashara na Uwekezaji inaeleza kuwa watu saba kwa kila 10 ya waliojihusisha na shughuli za viwanda walikuwa ni wanaume.
Hii ina maana kuwa idadi ya wanaume wanaojihusisha na shughuli za viwandani ni mara mbili zaidi ya wanawake, jambo linalofanya wanawake wawe nyuma zaidi kunufaika na fursa za sekta hiyo.